Latest News


More

JE WAJUA MADHARA YA NYAMA KWA AFYA YAKO?

Posted by : Unknown on : Tuesday, August 12, 2014 0 comments
Unknown
Saved under :

VYAKULA: Wengi hupenda nyama lakini wataalam wanatahadharisha




“Mtindo wa maisha na ulaji ni kati ya vitu vinavyowaathiri wengi hasa katika nchi zilizoendelea. Hata hivyo mtindo wa maisha wa kutozingatia ulaji na mpangilio wa vyakula ni kati ya vitu vinavyokuza magonjwa ya saratani ya tumbo, utumbo na njia ya haja kubwa.” Dk Halifa Mkumbi 

  • Afya ya binadamu katika nyakati hizi imekuwa hatarini kuliko miaka ya nyuma kutokana na maradhi kuongezeka. Hivyo watu wameanza kula vyakula kwa kuchukua tahadhari na umakini mkubwa.
0
Share
Chakula ni dawa, lakini chaweza kuwa sumu pia. Watu wengi wana desturi ya kula ili kufurahi na tumbo lijae. Wakati huo huo ulaji unaweza kuwa chanzo cha matatizo yatakayoathiri mwili, ingawa usafi ulizingatiwa katika maandalizi hadi matumizi.
Mojawapo ni aina nyingi ya kemikali ambazo mtu anaweza kuzitia tumboni kwa kivuli cha ‘chakula’ hivyo kuudhuru mwili.

Mwanataaluma wa Lishe, John Haule anasema chakula kinapoliwa na binadamu huwa na safari ndefu na husafiri kwa zaidi ya saa 13 hadi 72 kulingana na kile kilicholiwa.
“Utumbo mdogo au mwembamba una urefu mara nne ya urefu wa wastani wa mtu mzima. Unakadiriwa kuwa na urefu wa futi 18 hadi 23. Isingekuwa kwamba umesokotwa sokotwa kwa namna ya ajabu , usingeenea tumboni,” anasema.
Anafafanua kuwa tumbo limehifadhi vitu vingi na hivyo kuwa na uwezo wa kuweka mipaka na kupangilia umeng’enywaji wa chakula kinacholiwa kila siku na hicho ndicho hujenga na kuukarabati mwili wa binadamu.
“Tumbo la binadamu si kitu kidogo. Tumbo huweza kuhifadhi vyote unavyokula kila siku huku vingine vikikaa tumboni kwa hata saa 72 bila kuyeyuka, kwa sababu utumbo mwembamba tu wa binadamu una urefu wa futi 18 hadi 23 au mita saba ambazo ni takriban sawa na urefu wa nguzo ya umeme wa nyumbani,” anabainisha.
Anasema utumbo huo umeungana na utumbo mnene. Huu una urefu wa futi tatu au  futi tano.
“Kwa hiyo ukipima urefu wa utumbo wote utastaajabu sana maana utapata futi 27 au mita nane na nusu,” anasema Haule.
Wakati wa umeng’enyaji, anasema tumbo hukutana na kibarua kigumu pale mtu anapokula vyakula vinavyosindikwa viwandani ambavyo vina kemikali za kuvifanya visiharibike mapema.
Anatoa mfano wa kemikali hiyo ya kuhifadhi vyakula husababisha ukinzani wakati wa chakula kumeng’enywa tumboni na matokeo yake husababisha vitumie muda mrefu ili kusanisiwa mwilini.
Vyakula vya namna hiyo, kama vile nyama nyekundu na vile vilivyopikwa na mafuta mengi huweza kuchukua hadi saa 72, sawa na siku tatu kukamilisha kazi ya umeng’enyaji.
Mazingira hayo ya chakula kudumu muda mrefu husababisha sumu kwenye vyakula kuongezeka kama vile tindikali.

Anasema pia hujumuisha tindikali pamoja na vitu vingine hatari kwa afya kama mafuta, lehemu, chumvi na kafeini ambavyo huathiri ini.
“Kwenye ini ndiko mifumo mingine huathirika na mtu kujikuta akiugua maradhi ya moyo na damu kama vile shinikizo la damu, kisukari, kupooza na maradhi ya mara kwa mara,” anasema.
Mkurugenzi wa Kituo cha Huduma ya Ushauri Nasaha, Lishe na Afya, Mary Materu anasema kutozingatia ulaji unaofaa na mtindo bora wa maisha ni chanzo cha kupata magonjwa mengi yakiwamo saratani.
“Aina nyingi za saratani huanzia katika mtindo wa maisha na ulaji wa mhusika. Mtu anapokula vyakula vinavyoushughulisha utumbo mwembamba na mpana kuchuja vyakula hivyo kwa muda mrefu, husababisha maafa baadaye.

“Huanza kusababisha tumbo kujaa gesi, kuuma, kukosa haja na hata kukosa hamu ya kula,” anasema.
Viko baadhi ya vyakula vinavyoweza kuongeza uwezekano wa kupata saratani. Vyakula hivi mara nyingi ni vile vyenye mafuta mengi ambavyo vinasababisha uzito mkubwa na huweza kumfanya mtu kupata magonjwa ya saratani ya matiti, kongosho na kizazi,” anasema Materu.
Kuhusu nyama nyekundu yaani nyama ya mbuzi na ya ng’ombe, anasema ni moja ya sababu zinazosababisha tatizo hilo.

 “Nyama nyekundu ni muhimu sana kwa binadamu, lakini inapoliwa kupita kiasi ni tatizo.Kwa kawaida binadamu anatakiwa kula nusu kilo ya nyama kwa wiki, lakini walio wengi wanakula nusu kilo au zaidi kwa siku. Hilo ni tatizo,” anasema huku akishauri watu wapendelee kula nyama nyeupe.
“Nyama nyeupe ambayo ni samaki, kuku na dagaa ni muhimu sana kwa mwili na haina madhara sana kama ilivyo kwa nyama nyekundu ambayo ni ngumu katika kumeng’enywa hivyo kutumia muda mrefu.”
Hata hivyo wataalamu walioangalia tafiti nyingi zilizofanyika kuhusu nyama nyekundu na saratani, wameona upo uthibitisho wa kutosha kwamba ulaji wa nyama nyekundu kwa kiasi kikubwa unaongeza uwezekano wa kupata saratani ya utumbo mkubwa.

Tafiti huo umeonyesha kula hadi nusu kilo kwa wiki haiongezi uwezekano wa kupata saratani, lakini kila gramu 50 inayoongezeka hufanya uwezekano wa kupata saratani kwa asilimia 15.

Vyakula Vilivyosindikwa

Haule amezitaja nyama zilizosindikwa pamoja na vyakula vingine vya aina hiyo, hutumia muda mrefu kumeng’enywa.
 “Vyakula vilivyosindikwa vimethibitishwa kwamba vinaongeza uwezekano wa kupata saratani.  Hata hivyo, wataalamu wanasema hawajaweza kuona kiasi chochote cha nyama iliyosindikwa kinachoweza kutumika bila kuongeza uwezekano wa kupata saratani,” anasema Haule.   Nyama iliyosindikwa ni pamoja na ile iliyohifadhiwa kwa kuongezwa chumvi, mafuta, kemikali au kukaushwa kwa moshi. Aina hii ya nyama ni pamoja na nyama za kopo, soseji, bekoni na zinginezo.
Daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake na uzazi, Halifa Mkumbi anasema mtindo wa maisha na ulaji ni kati ya vitu vinavyowaathiri wengi hasa katika nchi zilizoendelea. Hata hivyo anasema mtindo wa maisha wa kutozingatia ulaji na mpangilio wa vyakula ni kati ya vitu vinavyokuza magonjwa ya saratani ya tumbo, utumbo na njia ya haja kubwa,” anasema.

Kukua kwa teknolojia pamoja na biashara, kumesababisha vyakula vya kusindikwa kutumika hadi maeneo ya vijijini ambako siku za nyuma vilikuwa havitumiki.
Kutokana na hali hiyo, magonjwa kama vile kisukari na maradhi ya moyo, yaliwapata zaidi watu wa mijini lakini siku hizi yameenea hadi maeneo ya vijijini.
Ili vyakula viweze kumeng’enywa vizuri, inashauriwa kula mbogamboga kwa wingi pamoja na matunda.

Katika upikaji wa mboga, inashauriwa zisipikwe sana ili kutoharibu viinilishe muhimu Ikiwezekana baadhi ya mboga ziliwe zikiwa mbichi ili kukamilisha lengo hilo.
(Source: Mwananchi communication)

No comments:

Leave a Reply