Latest News


More

JE SAYANSI INAPATANA NA BIBLIA?

Posted by : Unknown on : Saturday, September 13, 2014 0 comments
Unknown
Saved under :

Jibu la Biblia

Ndiyo, hata ingawa Biblia si kitabu cha kisayansi, inazungumzia mambo ya kisayansi kwa usahihi. Fikiria mifano fulani inayoonyesha kwamba sayansi inapatana na Biblia na kwamba Biblia yenyewe inataja mambo hakika ya kisayansi yanayotofautiana na yale ambayo watu walioishi zamani waliamini.
  • Ulimwengu ulikuwa na mwanzo. (Mwanzo 1:1) Tofauti na hilo, hekaya nyingi za kale zinasema kwamba ulimwengu haukuumbwa, ulijitokeza wenyewe. Wababiloni waliamini kwamba miungu iliyozaa ulimwengu ilitoka katika bahari mbili. Hekaya nyingine zinasema kwamba ulimwengu ulitoka katika yai kubwa sana.
  • Ulimwengu unaongozwa na sheria za asili, si utendaji wa miungu. (Ayubu 38:33; Yeremia 33:25) Hekaya mbalimbali ulimwenguni pote zinafundisha kwamba wanadamu hawawezi kufanya jambo lolote isipokuwa kile kilichoamuliwa na miungu inayotenda mambo yasiyotarajiwa na yenye ukatili.
  • Dunia inaelea angani. (Ayubu 26:7) Watu wengi walioishi nyakati za kale waliamini kwamba dunia ni tambarare na kwamba imeshikiliwa na jitu fulani au mnyama, kama vile nyati au kasa.
  • Maji yanayoingia katika mito na vijito huwa yamevukizwa kutoka baharini au kutoka katika vyanzo vingine kisha yanamwagika tena yakiwa mvua, theluji, au mvua ya mawe. (Ayubu 36:27, 28; Mhubiri 1:7; Isaya 55:10; Amosi 9:6) Wagiriki wa kale walifikiri kwamba maji ya mito yalitoka kwenye bahari iliyo chini ya ardhi, na wazo hilo liliendelezwa hadi karne ya 18.
  • Milima huibuka na kuporomoka, na wakati fulani milima iliyopo leo ilikuwa chini ya bahari. (Zaburi 104:6, 8) Tofauti na maoni hayo, hekaya fulani zinasema kwamba milima iko jinsi ilivyo leo kwa sababu iliumbwa na miungu.
  • Mazoea mazuri ya kutunza usafi hulinda afya. Sheria ambayo Waisraeli walipewa, ilitia ndani maagizo ya kwamba mtu anapaswa kuoga baada ya kugusa maiti, watu waliokuwa na magonjwa ya kuambukiza walipaswa kutengwa, na kinyesi kilipaswa kuzikwa. (Mambo ya Walawi 11:28; 13:1-5; Kumbukumbu la Torati 23:13) Tofauti na hilo, wakati ambapo sheria hizo zilikuwa zikitolewa, Wamisri walikuwa wakitumia mchanganyiko uliokuwa na kinyesi cha mwanadamu ili kutibu majeraha.

Je, kuna makosa ya kisayansi katika Biblia?

Mtu anayechunguza Biblia kwa akili iliyofunguka atajibu hapana. Yafuatayo ni maoni fulani yaliyo na kasoro ambayo watu hutoa kuonyesha Biblia si sahihi kisayansi:
Uwongo: Biblia inasema kwamba ulimwengu uliumbwa katika siku sita zenye urefu wa saa 24.
Ukweli: Biblia haitoi tarehe hususa ambayo Mungu aliumba ulimwengu. (Mwanzo 1:1) Pia, siku za uumbaji zinazofafanuliwa katika Mwanzo sura ya 1 ni kipindi cha wakati chenye urefu usiojulikana. Kwa kweli, kipindi chote cha wakati ambacho mbingu na dunia ziliumbwa kinaitwa “siku.”Mwanzo 2:4.
Uwongo: Biblia inasema kwamba mimea iliumbwa kabla ya jua ambalo husababisha mfumo wa usanidi-mwanga.Mwanzo 1:11, 16.
Ukweli: Biblia inaonyesha kwamba jua, mojawapo ya nyota zilizo katika “mbingu,” liliumbwa kabla ya mimea. (Mwanzo 1:1) Katika “siku” ya kwanza ya uumbaji, nuru ya jua ilipenya angani na kuanza kuonekana duniani. Anga lilipoendelea kuruhusu mwangaza huo uonekane waziwazi duniani, mfumo wa usanidi-mwanga ulianza kutenda kazi kwenye mimea katika “siku” ya tatu ya uumbaji. (Mwanzo 1:3-5, 12, 13) Baadaye ndipo jua lilipoonekana waziwazi kutoka duniani.Mwanzo 1:16.
Uwongo: Biblia inasema kwamba jua huzunguka dunia.
Ukweli: Andiko la Mhubiri 1:5 linasema: “Jua limechomoza, na kushuka, nalo linajitahidi kwa nguvu kwenda mahali pake ambapo litachomoza tena.” Maneno hayo yanategemea maoni ya mtu anayetazama jua kutoka duniani. Ni kama vile tu leo tunasema “jua limechomoza” na “jua limetua” hata ingawa ukweli wa mambo ni kwamba dunia ndiyo inayolizunguka jua.
Uwongo: Biblia inasema kwamba dunia ni tambarare.
Ukweli: Biblia inapozungumza kuhusu “miisho ya dunia” inamaanisha “sehemu ya mbali zaidi ya dunia”; maneno hayo hayamaanishi kwamba dunia ni tambarare wala ina mwisho. (Luka 11:31) Vivyo hivyo, maneno “miisho minne ya dunia” ni usemi wa mfano unaorejelea eneo lote la dunia na si kwamba dunia ina pembe nne.Isaya 11:12; Luka 13:29.
Uwongo: Biblia inasema kwamba mzingo wa mviringo au duara ni mara tatu ya kipenyo chake, lakini hesabu sahihi ni pai (π), au 3.1416 hivi.
Ukweli: Vipimo vinavyotajwa katika 1 Wafalme 7:23 na 2 Mambo ya Nyakati 4:2 vinaonyesha kwamba “Bahari ya kuyeyushwa” ilikuwa na kipenyo cha mikono 10 na kwamba “kamba ya urefu wa mikono 30 ingeweza kuizunguka pande zote.” Huenda vipimo hivyo vilikuwa tu vya kukadiria. Huenda pia mzingo ulipimwa kwa kutegemea sehemu ya nje ya bahari hiyo huku kipenyo kikitegemea upande wake wa ndani.
(Source: http://www.jw.org)

No comments:

Leave a Reply