Latest News


More

WAZAZI WANGU HAWANIAMINI - NIFANYEJE?

Posted by : Unknown on : Saturday, September 13, 2014 0 comments
Unknown
Saved under :

Wazazi Wangu Hawaniamini

Unachoweza kufanya

Fikiria: Kwa ujumla, je, mwenendo wako unawapa wazazi wako sababu yoyote ya kutokukuamini?
Kwa mfano, mtume Paulo aliandika: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Jiulize, ‘Nimejiwekea rekodi ya aina gani inapohusu kuwaambia wazazi wangu ukweli kuhusu mahali nilipo na mambo ninayofanya?’

Lori

 Kwa siri nilikuwa nikimtumia barua-pepe kijana fulani niliyempenda. Wazazi wangu waligundua na kuniambia niache. Niliahidi nitaacha, lakini sikuacha. Niliendelea kufanya hivyo kwa mwaka mzima. Ningemtumia barua-pepe, kisha wazazi wangu wangegundua nami ningeomba msamaha na kuwaahidi kwamba nitaacha, lakini bado ningeendelea. Ilifikia hatua ambapo wazazi wangu hawangeweza kuniamini tena!
Unafikiri ni kwa nini wazazi wa Lori waliacha kumwamini?
Ikiwa Lori angekuwa binti yako, ungefanya nini, na kwa nini?
Lori angetendaje wazazi wake walipozungumza naye mara ya kwanza?

Beverly

 Wazazi wangu hawakuamini kwamba ningetenda kwa njia inayofaa kuelekea wavulana, lakini sasa ninaelewa kwa nini walifanya hivyo. Tulikuwa tukichezeana kimapenzi na wavulana kadhaa waliokuwa na umri wa miaka miwili zaidi yangu. Nilikuwa nikizungumza nao kwa muda mrefu kwenye simu, na katika vikusanyiko mbalimbali ningezungumza nao peke yao. Wazazi wangu walininyang’anya simu kwa mwezi mmoja, na hawakuniruhusu niende mahali vijana hao wangekuwa.
Ikiwa Beverly angekuwa binti yako, ungefanya nini, na kwa nini?
Unafikiri masharti ambayo wazazi wa Beverly walimwekea yalipita kiasi? Ikiwa unafikiri hivyo, ni kwa nini?
Beverly angeweza kufanya nini ili wazazi wake waanze kumwamini tena?

Kuanza Kuaminiwa Tena

Unachoweza kufanya

Kwanza, tambua umeacha kuaminika kuhusiana na mambo gani.
Hatua ya kuwa mtu mzima anayeaminika ni kama kupanda ngazi, hatua kwa hatua, miaka yote unapokua
  • Kufika nyumbani wakati niliowekewa na wazazi
  • Kufanya mambo kwa wakati
  • Kumaliza kazi
  • Kudumisha chumba changu kikiwa safi
  • Kutumia simu
  • Kutimiza ahadi zangu
  • Kutumia pesa kwa hekima
  • Kuamka bila kubembelezwa
  • Kusema kweli
  • Kukubali makosa na kuomba msamaha
  • Mambo mengine
Pili, fanya azimio. Jiwekee lengo la kuwa mwaminifu katika mambo uliyotia alama. Fuata himizo hili la Biblia: ‘Ondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wako wa kwanza.’ (Waefeso 4:22) Baada ya muda, maendeleo yako yataonekana wazi kwa kila mtu, kutia ndani wazazi wako.—1 Timotheo 4:15.
Tatu, zungumza na wazazi wako kuhusu azimio lako. Badala ya kulalamika kwamba wanahitaji kukuamini zaidi, waulize kwa heshima wangependa ufanye nini ili wakuamini.
Tahadhari: Usitazamie wazazi wako wakuondolee vizuizi mara moja. Bila shaka, wangependa kuhakikisha kwamba utatimiza ahadi zako. Tumia nafasi uliyo nayo kujithibitisha kuwa mwenye kuaminika. Muda si muda, wazazi wako watakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Beverly aliyetajwa awali. “Inachukua muda mrefu kumwamini mtu, lakini ni rahisi sana kuacha kumwamini,” akasema huku akiongezea hivi, “nimeanza kuaminiwa sasa, na ninahisi vizuri!”
Ukweli wa mambo: Kadiri unavyotegemeka, ndivyo utakavyoaminika zaidi.
(Source: http://www.jw.org)

No comments:

Leave a Reply