Latest News


More

MTOTO ANAWEZAJE KUBORESHA NDOA

Posted by : Unknown on : Thursday, March 26, 2015 0 comments
Unknown
Saved under :
“Wana ni urithi kutoka kwa Yehova.” Zaburi 127:3
Mtoto anapozaliwa, huenda kikawa kipindi cha kusisimua na chenye mkazo kwa mume na mke. Mkiwa wazazi wapya, huenda mkatumia muda mwingi kumtunza na kumlea mtoto wenu. Huenda kukosa usingizi na mabadiliko ya kihisia yakaleta mkazo kwenye ndoa yenu. Nyote wawili mnapaswa kufanya marekebisho ili mfanikiwe kumlea mtoto na pia kudumisha ndoa yenu. Ushauri wa Biblia unawezaje kuwasaidia mfanikiwe?

 1 ELEWA JINSI MTOTO ANAVYOBADILI MAISHA YENU

BIBLIA INASEMA HIVI: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” Pia, upendo “hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Ukiwa mama mpya, utatumia muda mwingi kumtunza mtoto wako. Hata hivyo, huenda mume wako akaanza kuhisi amepuuzwa, kwa hiyo usisahau kwamba yeye pia anahitaji kukaziwa fikira. Kwa subira na fadhili, unaweza kumsaidia ahisi anathaminiwa na anahusika katika kumlea mtoto wenu.
Baba akimlisha mtoto chakula, na akimtunza wakati wa usiku
“Enyi waume, endeleeni kukaa nao . . . kulingana na ujuzi.” (1 Petro 3:7) Elewa kwamba mke wako atatumia muda mwingi kumtunza mtoto wenu. Kwa sababu ana jukumu jipya huenda akawa na mkazo, uchovu na hata kushuka moyo. Nyakati nyingine, huenda akakukasirikia, lakini uwe mtulivu, kwa sababu mtu “asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu.” (Methali 16:32) Uwe mwenye utambuzi na umpe msaada anaohitaji. Methali 14:29.
UNACHOWEZA KUFANYA:
  • Baba: Msaidie mke wako kumtunza mtoto, hata kama ni usiku. Punguza muda unaotumia kufanya mambo mengine ili upate muda zaidi wa kuwa na mkeo pamoja na mtoto
  • Mama: Mume wako anapojitolea kumtunza mtoto, kubali msaada wake. Ikiwa hafanyi vizuri, usimkosoe, badala yake kwa fadhili mwelekeze jinsi anavyopaswa kufanya

 2 IMARISHENI UHUSIANO WENU

BIBLIA INASEMA HIVI: “Watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Ingawa mmepata mtu mpya kwenye familia yenu, kumbuka kwamba wewe na mwenzi wako bado ni “mwili mmoja.” Jitahidini kuimarisha uhusiano wenu.
Mke, mshukuru mume wako kwa msaada na utegemezo wake. Maneno yako ya shukrani yanaweza ‘kuponya.’ (Methali 12:18) Mume, mwambie mke wako jinsi unavyompenda na kumthamini. Mpongeze mkeo kwa jinsi anavyoitunza familia.Methali 31:10, 28.
Mume na mke wakiwa pamoja wakati mtoto wao amelala
“Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Sikuzote jitahidi kumfanyia mwenzi wako mambo mema. Uwe na muda wa kuzungumza, kumpongeza, na kumsikiliza mwenzi wako. Msinyimane uhusiano wa kingono. Zingatia mahitaji ya mwenzi wako. Biblia inasema hivi: “Msiwe mkinyimana haki hiyo, ila kwa makubaliano.” (1 Wakorintho 7:3-5) Zungumzieni jambo hilo kwa unyoofu nyinyi wenyewe. Mkionyesha subira na utambuzi mtaimarisha ndoa yenu.
UNACHOWEZA KUFANYA:
  • Msisahau kupanga wakati wa kuwa pamoja peke yenu
  • Usisahau kufanya mambo yatakayomwonyesha mwenzi wako kwamba unampenda, kama vile kumtumia ujumbe au kumnunulia zawadi

 3 KUMZOEZA MTOTO WENU

Mama akimsomea  mtoto wake kitabu
BIBLIA INASEMA HIVI: “Tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.” (2  Timotheo 3:15) Pangeni mapema jinsi mtakavyomfundisha mtoto wenu. Mtoto ana uwezo mkubwa wa kujifunza hata kabla hajazaliwa. Anapokuwa tumboni, mtoto anaweza kutambua sauti na hisia zako. Msomee hata akiwa bado mchanga. Hata kama hataelewa unachosoma, hilo litamsaidia kupenda kusoma atakapokuwa mkubwa.
Mtoto wako anaweza kuelewa unapozungumza kuhusu Mungu. Mwache asikie unaposali kwa Yehova. (Kumbukumbu la Torati 11:19) Hata unapocheza na mtoto wako, zungumza kuhusu vitu ambavyo Mungu ameumba. (Zaburi 78:3, 4) Kadiri mtoto wako anavyokua atatambua jinsi unavyompenda Yehova naye pia atajifunza kumpenda.
UNACHOWEZA KUFANYA:
  • Mwombe Yehova akupe hekima ya kumfundisha mtoto wako
  • Mtajie mtoto wako tena na tena maneno na mawazo makuu ili aanze kujifunza mapema

Saved under :

No comments:

Leave a Reply