Latest News


More

Kardinali Pengo amjibu Askofu Gwajima

Posted by : Unknown on : Wednesday, April 1, 2015 0 comments
Unknown
Saved under :


Dar es Salaam.
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amesema, amemsamehe Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima ambaye hivi karibuni alimtolea maneno makali kutokana na kutofautiana naye juu ya msimamo wa viongozi wa Kikristo kuhusu Katiba Inayopendekezwa.
Kardinali Pengo alitoa msamaha huo mbele ya waumini katika Kanisa la St Joseph, Dar es Salaam jana, siku mbili baada ya Askofu Gwajima kuhojiwa na Polisi kwa madai ya kumkashifu kiongozi huyo, mbele ya hadhara.
Askofu Gwajima anadaiwa kutoa kauli za kumkashifu kiongozi huyo kwamba amewasaliti wa viongozi wenzake wa Kikristo kwa kuwataka waumini wa dini hiyo kuamua wenyewe suala la Katiba Inayopendekezwa kinyume na msimamo wa waraka wa kupinga katiba hiyo uliotolewa na Jukwaa la Wakristo Tanzania (CCT).
Baada ya kutolewa kwa waraka huo ulioagiza waumini kuipigia kura ya hapana katiba hiyo, Askofu Pengo alinukuliwa akisema viongozi wa dini hawana mamlaka ya kuzuia wananchi kuikubali Katiba hiyo huku akisisitiza waachiwe uhuru wao wa kuamua.
Akizungumza jana wakati wa ibada ya Jumapili ya Matawi, inayoadhimishwa wiki moja kabla ya Sikukuu ya Pasaka, Kardinali Pengo, bila ya kumtaja jina alisema: “Natumia nafasi hii kueleza juu ya maneno ambayo yalitolewa na mchungaji fulani, sikumbuki anaitwa nani… nasema nimemsamehe kutoka ndani ya moyo wangu wote, anaweza kuwa na sababu zake ila nimemsamehe kabisa.
“Sina ghadhabu wala chuki ila kinyume chake, naomba tumwombee yeye na watu wote waliokuwa wamehusika pengine nyuma yake ili Mungu aweze kutulinda na kutudumisha katika hali ya amani ya Taifa letu.”
Alisema hatua ya Polisi kumkamata ni sehemu ya kutekeleza utaratibu wa jeshi hilo tu, lakini yeye kwa nafsi yake ameshamsamehe.
Atolewa ICU, wafuasi wakamatwa
Katika hatua nyingine, Askofu Gwajima ametolewa kwenye chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) na kuhamishwa katika wodi ya kawaida  baada ya afya yake kuendelea vizuri.
Askofu huyo alikuwa ICU kwenye Hospitali ya TMJ, Mikocheni, alikofikishwa usiku wa Ijumaa baada ya hali yake kubadilika ghafla alipokuwa akihojiwa Kituo Kikuu cha Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam.
Askofu huyo alijisalimisha kituoni hapo akiitikia wito wa polisi uliomtaka kufanya hivyo kutokana na tuhuma za kutoa lugha chafu dhidi ya Kardinali Pengo.
Akizungumza jana, mke wa Askofu huyo, Grace Gwajima alisema baada ya madaktari kumuona anaendelea vizuri, wameamua kumtoa ICU na kumpeleka kwenye wodi ya kawaida.

(Source: Mwananchi Communication)

No comments:

Leave a Reply