Latest News


More

KILEO: Je ni vibaya kunywa kileo?

Posted by : Unknown on : Tuesday, August 27, 2013 0 comments
Unknown
Saved under :



Je, ni vibaya kunywa kileo?

“Divai ya kumchangamsha, mafuta ya zeituni ya kumfurahisha, na mkate wa kumpa nguvu.”—Zaburi 104:15, “Biblia Habari Njema.”

WATU HUSEMA NINI?

Katika nyumba nyingi, ni jambo la kawaida kunywa kileo wakati wa mlo. Katika nyumba nyingine, hairuhusiwi. Kwa nini kuna maoni hayo tofauti? Maoni ya watu yanaathiriwa na mambo mbalimbali kama vile utamaduni, afya, na dini.
BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inakataza ulevi na kunywa kileo kupita kiasi lakini haikatazi kutumia kileo kwa kiasi. (1 Wakorintho 6:9, 10) Kwa kweli, tangu zamani za kale, waabudu wa Mungu—wanaume na wanawake—walikunywa divai, kileo kinachotajwa zaidi ya mara mia mbili katika Biblia. (Mwanzo 27:25) ‘Ule chakula chako kwa kushangilia na kunywa divai yako kwa moyo mchangamfu,’ inasema Mhubiri 9:7. Kwa sababu divai hufanya moyo ushangilie, mara nyingi iliandaliwa wakati wa sherehe, kama vile katika karamu za arusi. Yesu alifanya muujiza wake wa kwanza katika karamu ya arusi alipogeuza maji kuwa “divai nzuri.” (Yohana 2:1-11) Divai pia ilitumiwa kama dawa.—Luka 10:34; 1 Timotheo 5:23.
Je, Biblia inaweka mipaka ya kiwango cha kileo ambacho mtu anapaswa kunywa?

“[Msiwe] watumwa wa divai nyingi sana.”—Tito 2:3.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Kila mwaka, familia nyingi huteseka kwa sababu mzazi mmoja au wote wawili hunywa kileo kupindukia. Pia, kwa sababu ya kunywa kupindukia, watu wengi huanguka na kuumia, wengine husababisha aksidenti, kutia ndani aksidenti za barabarani. Utumizi mbaya wa kileo kwa muda mrefu unaweza kudhuru ubongo, moyo, ini, na tumbo
BIBLIA INASEMA NINI?

Kunywa na kula kwa kiasi ni takwa la msingi kutoka kwa Mungu. (Methali 23:20; 1 Timotheo 3:2, 3, 8) Mtu asiyeweza kujizuia hawezi kuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Biblia inasema hivi: “Divai ni mdhihaki, kileo husababisha msukosuko, na kila mtu anayepotezwa nacho hana hekima.”—Methali 20:1.
Njia moja ambayo kileo kinaweza kumpoteza mtu asiye na hekima ni kwa kudhoofisha msimamo wake thabiti wa maadili. Andiko la Hosea 4:11 linasema hivi: “Divai na divai tamu ndivyo vinavyoondoa kusudi jema.” Mwanamume anayeitwa John alijifunza hilo kwa majonzi. * Alipogombana na mke wake, alienda kwenye hoteli fulani, akanywa kileo kupita kiasi, na kufanya uzinzi—alijuta sana baadaye na akaazimia kwamba hatarudia tena kufanya hivyo. Kutumia vibaya kileo kunaweza kutudhuru kimwili, kiadili, na kiroho, na Biblia inasema kwamba walevi hawataurithi uzima wa milele.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Ni wakati gani ambapo haifai kunywa kileo?

“Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.”—Methali 22:3, “Biblia Habari Njema.”

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

“Kileo ni dawa ya kulevya yenye nguvu sana,” kinasema kitabu World Book Encyclopedia. Kwa hiyo, huenda kutakuwa na pindi au nyakati ambapo si jambo la hekima kunywa kileo hata kwa kiasi.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mara nyingi watu “hujitokeza mbele” na kuingia matatani kwa sababu ya kunywa kileo wakati usiofaa. Biblia inasema kwamba “kuna wakati uliowekwa wa kila kitu,” kutia ndani wakati wa kujiepusha na kileo. (Mhubiri 3:1) Kwa mfano, huenda mtu asiwe amefikisha umri unaoruhusiwa kisheria kunywa kileo, huenda zamani alikuwa mraibu wa kileo, au huenda anatumia dawa ambazo zinaweza kumdhuru zikitumiwa pamoja na kileo. Na kwa watu wengi, “wakati uliowekwa” wa kujiepusha na kileo ni kabla ya kwenda kazini na wakiwa kazini, hasa ikiwa wanatumia mashine hatari. Kwa kweli, watu wenye hekima huona uhai na afya kuwa zawadi zenye thamani kutoka kwa Mungu. (Zaburi 36:9) Tunaheshimu zawadi hizo tunapoacha kanuni za Biblia zituongoze kuhusiana na matumizi ya kileo.

No comments:

Leave a Reply