Latest News


More

Ponografia - Je, Ina Madhara?

Posted by : Unknown on : Thursday, August 15, 2013 0 comments
Unknown
Saved under :
Ponografia—Je, Ina Madhara?


Ponografia imesambaa ulimwenguni pote. * Inapatikana kwenye matangazo ya biashara, mitindo, sinema, muziki, na magazeti, vilevile kwenye televisheni, michezo ya video, simu, vifaa vya kielektroniki vinavyobebwa, na pia kwenye Intaneti. Inaonekana ponografia inapendwa na watu wengi sana. Watu wengi zaidi katika maeneo mbalimbali wanatazama ponografia kuliko wakati mwingine wowote katika historia.

Ponografia inazidi kubadilika. Profesa Gail Dines anaandika hivi: “Leo, picha zinazidi kuwa mbaya hivi kwamba ponografia iliyoonwa kuwa chafu sana imekuwa ya kawaida.”

Wewe una maoni gani? Je, ni sawa kutazama ponografia, ni hatari, au huna msimamo wowote? Yesu alisema: “Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa.” (Mathayo 7:17) Ponografia hutokeza matunda ya aina gani? Ili tupate jibu, acheni tuchunguze maswali fulani ya msingi kuhusu ponografia.

Ponografia inawaathirije watu wanaoitazama?

WATAALAMU HUSEMA: Watu wanaotazama ponografia huwa na mazoea sugu ya kuitazama, na watafiti fulani huilinganisha na kutumia kokeini kali.

Brian, * ambaye alikuwa na mazoea ya kutazama ponografia kwenye Intaneti anasimulia: “Hakuna kitu ambacho kingenizuia. Ni kana kwamba nilikuwa katika ulimwengu mwingine. Nilitetemeka na kuhisi maumivu kichwani. Nilijitahidi kuacha, lakini niliendelea kutazama kwa miaka mingi.”

Mara nyingi, watu wanaotazama ponografia huficha zoea hilo. Ni wasiri na pia wadanganyifu. Si ajabu kwamba wengi wao huhisi upweke, huona aibu, hushuka moyo, huwa na wasiwasi, na kukasirika. Hata wengine wao hutamani kujiua. “Nilijitenga na watu na kukata tamaa,” anasema Serge ambaye alitazama ponografia kwenye simu yake ya mkononi karibu kila siku. “Nilijihisi mwenye hatia, asiyefaa, mpweke, na aliyenaswa. Niliaibika sana na nikaogopa kutafuta msaada.”

Hata kutazama ponografia kifupi bila kukusudia kunaweza kuwa na madhara. Akitoa ushahidi mbele ya kamati ya Seneti ya Marekani, mtafiti wa mambo ya ponografia Dkt. Judith Reisman alisema: “Picha za ponografia hubaki akilini, na kuhifadhiwa kwa njia ya kudumu ambayo hutokeza kumbukumbu ambazo ni vigumu au haziwezi kufutwa.” Susan mwenye umri wa miaka 19 ambaye alitazama Tovuti za ponografia anasema: “Bado picha hizo ziko akilini. Mimi huzikumbuka bila kutaka. Ninahisi kwamba sitafaulu kamwe kuzifuta kabisa.”

JAMBO HAKIKA: Ponografia hutokeza mazoea sugu na huwaathiri watu wanaoitazama.—2 Petro 2:19.

Ponografia huathirije familia?

WATAALAMU HUSEMA: “Ponografia huvunja ndoa na familia.”—Kitabu The Porn Trap, cha Wendy na Larry Maltz.

Ponografia huharibu ndoa na familia kwa:

• Kusababisha kutoaminiana, kuvuruga upendo na mapenzi.—Methali 2:12-17.

• Kusababisha ubinafsi, mtengano wa kihisia, na kutoridhika na mwenzi wa ndoa.—Waefeso 5:28, 29.

• Kuchochea mawazo na hamu ya ngono haramu.—2 Petro 2:14.

• Kumshawishi mtazamaji amlazimishe mwenzi wake kufanya ngono kwa njia isiyo ya kawaida.—Waefeso 5:3, 4.

• Kuendeleza ukosefu wa uaminifu wa kihisia na kimwili.—Mathayo 5:28.

Biblia huwashauri wenzi wa ndoa ‘wasitendeane kwa hila.’ (Malaki 2:16) Ukosefu wa uaminifu ni hila ambayo inaweza kuvuruga ndoa na kusababisha kutengana na talaka. Ndoa inapovunjika, watoto huteseka sana.

Ponografia inaweza pia kuwaathiri watoto moja kwa moja. Brian aliyetajwa mapema, anasema: “Nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, nilipata magazeti ya baba yenye picha za ponografia tulipokuwa tukicheza. Nilianza kuyatazama kisiri, bila kuelewa hasa kwa nini nilivutiwa na picha hizo. Nikawa na zoea baya lililoendelea kwa miaka mingi.” Uchunguzi unaonyesha kwamba ponografia inaweza kuwashawishi vijana waanze kufanya ngono wakiwa na umri mdogo na pia kuwa na maadili mapotovu, kuwa wajeuri kingono, na kuvurugika kihisia na kisaikolojia.

JAMBO HAKIKA: Ponografia huharibu uhusiano katika familia na kusababisha maumivu na uchungu mwingi.—Methali 6:27.

Biblia inasema nini kuhusu ponografia?

NENO LA MUNGU LINASEMA: “Viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”—Wakolosai 3:5.

Kwa ufupi, Yehova * Mungu anachukia ponografia. Hilo halimaanishi kwamba anachukia mambo ya ngono. Ndiye aliyeumba uwezo wetu wa kingono na kukusudia mume na mke wautumie kufurahishana, kukaribiana kihisia, na kushirikiana kuzaa watoto.—Yakobo 1:17.

Kwa nini basi Yehova anachukia sana ponografia? Acheni tuchunguze sababu chache.

• Anajua ponografia inaweza kuharibu maisha ya watu.—Waefeso 4:17-19.

• Anatupenda na anataka kutulinda tusipate madhara.—Isaya 48:17, 18.

• Yehova anataka kulinda ndoa na familia.—Mathayo 19:4-6.

• Anataka tuwe na maadili safi na tuheshimu haki za wengine.—1 Wathesalonike 4:3-6.

• Anataka tuheshimu uwezo wetu wa ngono na kuutumia kwa njia yenye kuheshimika.—Waebrania 13:4.

• Yehova anajua ponografia huendeleza mawazo ya kibinafsi, ya kishetani, na yaliyopotoka kuhusu ngono.—Mwanzo 6:2; Yuda 6, 7.

JAMBO HAKIKA: Ponografia huharibu uhusiano wa mtu pamoja na Mungu.—Waroma 1:24.

Hata hivyo, Yehova anawahurumia wale ambao wangependa kuacha kutazama ponografia. Biblia inasema: “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:8, 14) Anawasihi watu wanyenyekevu wamwendee ili ‘wapokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.’—Waebrania 4:16;

Watu wengi wamekubali msaada wa Mungu. Je, wamefaidika? Ona kile ambacho Biblia inasema kuhusu watu walioshinda mazoea mabaya: “Mmeoshwa mkawa safi, . . . mmetakaswa, . . . mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:11) Kama mtume Paulo, watu kama hao wanaweza kusema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.

Susan, aliyeshinda zoea la kutazama ponografia, anasema: “Yehova tu ndiye anayeweza kukuweka huru. Ukimwomba msaada na mwongozo, unaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Hatakuacha kamwe.”

No comments:

Leave a Reply