Latest News


More

JE BIBLIA INAJIPINGA YENYEWE?

Posted by : Unknown on : Saturday, September 13, 2014 0 comments
Unknown
Saved under :


Jibu la Biblia

Hapana, Biblia ina upatano tangu mwanzo hadi mwisho. Ingawa huenda baadhi ya mistari ya Biblia ikaonekana kuwa inajipinga yenyewe, kanuni zifuatazo zinaweza kutusaidia kuielewa vizuri mistari hiyo:
  1. Chunguza muktadha. Maneno ya mwandishi yeyote yule yanaweza kuonwa kuwa yanajipinga yenyewe au hayana upatano ikiwa yule anayeyasoma hajachukua hatua ya kuchunguza muktadha.
  2. Chunguza mtazamo wa mwandishi. Huenda watu waliojionea tukio fulani wakasimulia tukio hilo kwa usahihi kabisa lakini wasitumie maneno yaleyale kulisimulia au wasitaje habari zilezile.
  3. Zingatia desturi na mambo ya kihistoria yanayohusiana na mistari unayosoma.
  4. Tambua kwamba neno fulani linaweza kuwa na maana ya mfano na maana halisi.
  5. Tambua kwamba mtu anaweza kuhusianishwa na jambo fulani hata ingawa mtu huyo hakuhusika kibinafsi au moja kwa moja kulifanya jambo lenyewe. *
  6. Tumia Biblia iliyotafsiriwa kwa usahihi.
  7. Epuka kupatanisha mafundisho ya Biblia na mawazo au mafundisho yasiyofaa ya kidini.
Mifano ifuatayo itatusaidia kuelewa jinsi kuzingatia kanuni hizo kunavyoweza kutufanya tuelewe baadhi ya mambo katika Biblia ambayo huenda yakaifanya Biblia ionwe kuwa inajipinga yenyewe.

Kanuni ya 1: Muktadha

Ikiwa Mungu alipumzika katika siku ya saba, ni katika njia gani anaendelea kufanya kazi? Muktadha wa simulizi la uumbaji katika kitabu cha Mwanzo unaonyesha kwamba maneno Mungu “akaanza kupumzika siku ya saba kutokana na kazi yake yote ambayo alikuwa ameifanya” yanarejezea kihususa kazi yake ya kuumba dunia. (Mwanzo 2:2-4) Yesu hakuwa akipinga maneno hayo aliposema kwamba Mungu “anaendelea kufanya kazi mpaka sasa.” Alikuwa akizungumzia kazi nyingine ambazo Mungu anafanya, na wala si kazi ya uumbaji. (Yohana 5:17) Kazi za Mungu zinatia ndani kuongoza katika uandikaji wa Biblia na pia kuwatunza na kuwapa mwongozo wanadamu.Zaburi 20:6;105:5; 2 Petro 1:21.

Kanuni ya 2 na ya 3: Historia na mtazamo wa mwandishi

Yesu amponya mwanamume kipofu
Yesu alikuwa wapi alipomponya yule mwanamume kipofu? Kitabu cha Luka kinasema kwamba Yesu alimponya mwanamume kipofu, Yesu “alipokuwa akikaribia Yeriko,” ilhali simulizi hilohilo katika kitabu cha Mathayo linataja kwamba Yesu aliwaponya wanaume wawili vipofu, Yesu alipokuwa ‘akienda kutoka Yeriko.’ (Luka 18:35-43; Mathayo 20:29-34) Masimulizi yote mawili ambayo yaliandikwa na waandishi wawili wenye mtazamo tofauti, yanatupatia habari tofauti zinazokamilishana. Kuhusu idadi ya wanaume hao vipofu, Mathayo anataja kihususa kwamba walikuwa wanaume wawili, ilhali Luka alielekeza fikira zake kwa mwanamume ambaye Yesu alizungumza naye. Kuhusu suala la mahali, wachimbuaji wa vitu vya kale wamegundua kwamba Yeriko la siku za Yesu lilikuwa jiji lenye sehemu mbili, yaani, jiji la kale la Kiyahudi ambalo lilikuwa kilomita moja na nusu hivi kutoka kwenye jiji la karibuni la Kiroma. Kwa hiyo, huenda Yesu alifanya muujiza huo alipokuwa umbali fulani kati ya majiji hayo mawili.

Kanuni ya 4: Maana ya mfano na maana halisi ya maneno

Je, dunia itaangamizwa? Katika kitabu cha Mhubiri 1:4, Biblia inasema “dunia hudumu daima,” maneno ambayo yanaonwa na watu wengine kuwa yanapingana na mstari mwingine wa Biblia unaosema “nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.” (2 Petro 3:10Union Version) Hata hivyo, katika Biblia, neno “dunia” hutumiwa kihalisi kumaanisha sayari yetu na pia linatumiwa katika njia ya mfano kurejelea watu wanaoishi ndani yake. (Mwanzo 1:1; 11:1) Maangamizi ya “dunia” yanayotajwa katika andiko la 2 Petro 3:10 yanarejelea, si kuteketezwa kwa sayari yetu, bali “kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”2 Petro 3:7.

Kanuni ya 5: Tambua mhusika

Huko Kapernaumu, ni nani aliyetumwa na ofisa Mroma wa kijeshi ili amsihi Yesu aje kumsaidia? Kitabu cha Mathayo 8:5, 6 kinasema ofisa huyo Mroma wa kijeshi alimjia Yesu moja kwa moja kibinafsi, ilhalikitabu cha Luka 7:3 kinasema kwamba ofisa huyo aliwatuma wanaume wazee wa Wayahudi. Mistari hii ambayo huonekana kuwa inajipinga waziwazi inaweza kueleweka kwa kuzingatia kwamba ofisa mwenyewe alimsihi Yesu kwa sababu alipeleka maombi yake kupitia wazee ambao walikuwa wasemaji wake.

Kanuni ya 6: Tafsiri sahihi

Je, sisi sote ni watenda dhambi? Biblia inafundisha kwamba sisi sote tulirithi dhambi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. (Waroma 5:12) Inaonekana kwamba tafsiri nyingine za Biblia hupinga hoja hiyo kwa kusema kwamba mtu mzuri “hatendi dhambi.” (1 Yohana 3:6Biblia Habari Njema; Union Version) Hata hivyo, katika lugha ya awali, kitenzi cha Kigiriki cha neno “dhambi” katika andiko la 1 Yohana 3:6 kiko katika hali ya wakati uliopo, ambapo kwa kawaida katika lugha hiyo neno hilo linaonyesha kitendo kinachoendelea. Kuna tofauti kati ya dhambi tuliyorithi, ambayo hatuwezi kuiepuka, na zoea la kuvunja sheria za Mungu kimakusudi. Kwa sababu hiyo, tafsiri nyingine za Biblia zinajitahidi kuondoa utata huo zinapotumia maneno kama vile mtu asiye na “mazoea ya kufanya dhambi.”New World Translation.

Kanuni ya 7: Fuata Biblia, si mafundisho ya kidini yasiyo sahihi

Je, Yesu ni sawa na Mungu au ana cheo cha chini kuliko Mungu? Yesu alisema: “Mimi na Baba ni kitu kimoja,” maneno ambayo yanaonekana kuwa yanapingana na maneno mengine yanayosema “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 10:30; 14:28) Ili kuelewa vizuri mistari hiyo ya Biblia, tunapaswa kuchunguza yale ambayo Biblia inasema kumhusu Yehova na Yesu badala ya kujaribu kulinganisha au kupatanisha mawazo ya Biblia na fundisho la dini ya uwongo kuhusuUtatu. Biblia inafundisha kwamba Mungu ambaye Yesu mwenyewe anamwabudu anaitwa Yehova na kwamba Yehova ni baba yake pia. (Mathayo 4:10; Marko 15:34; Yohana 17:3; 20:17; 2 Wakorintho 1:3) Yesu si sawa na Mungu.
Muktadha wa maneno ya Yesu “Mimi na Baba ni kitu kimoja” unaonyesha kwamba alikuwa akizungumzia umoja katika maana ya kwamba yeye na Baba yake, Yehova Mungu, wana kusudi moja au malengo yaleyale. Hata baadaye Yesu alisema: “Baba yuko katika muungano pamoja na mimi, nami niko katika muungano pamoja na Baba.” (Yohana 10:38) Yesu aliwasaidia wafuasi wake wawe na kusudi na malengo kama yake kwani alimwambia hivi baba yake kuwahusu katika sala: “Nimewapa utukufu ambao umenipa, ili wapate kuwa kitu kimoja kama vile sisi tulivyo kitu kimoja. Mimi katika muungano pamoja na wao na wewe katika muungano pamoja na mimi.”Yohana 17:22, 23.

No comments:

Leave a Reply