Latest News


More

Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

Posted by : Unknown on : Tuesday, August 27, 2013 0 comments
Unknown

Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?


HARRIET alipokufa mwaka wa 2006, alikuwa na umri wa miaka 175 hivi. Ni wazi kwamba Harriet hakuwa mwanadamu. Alikuwa kobe wa Visiwa vya Galapagos aliyekuwa akiishi katika bustani ya wanyama nchini Australia. Akilinganishwa na sisi, Harriet aliishi muda mrefu sana. Lakini akilinganishwa na viumbe wengine, urefu wa maisha yake haukuwa jambo lisilo la kawaida. Fikiria mifano ifuatayo.
Watafiti nchini Finland wanasema kwamba kome anayetokeza lulu ambaye huishi katika maji baridi, anaweza kuishi kwa miaka 200.
Kwa kawaida, chaza anayechimba (ocean quahog) huishi zaidi ya miaka 100 na hata imesemekana kwamba kuna wale ambao wameishi zaidi ya miaka 400.
Miti mbalimbali kama vile sequoia, msonobari unaoitwa bristlecone, aina fulani za mvinje, na msonobari unaoitwa spruce, huishi kwa maelfu ya miaka.
Hata hivyo, wanadamu ambao wanaonwa kuwa viumbe wa hali ya juu zaidi duniani wanaweza kutumaini kuishi kwa miaka 80 au 90 tu licha ya kufanya jitihada nyingi kujaribu kurefusha maisha yao!

Una maoni gani—miaka 80 hivi ndio muda mrefu zaidi tunaoweza kuishi? Au je, kuna uwezekano wa kuishi muda mrefu zaidi? Watu wengi wanatumaini kwamba sayansi na teknolojia ya kitiba itatuonyesha njia ya kuishi muda mrefu zaidi.
Je, Sayansi Ina Suluhisho?

Sayansi imechangia sana kuboresha afya na teknolojia ya kitiba. “Ni watu wachache sana [nchini Marekani] wanaokufa kutokana na magonjwa ya kuambukiza au matatizo yanayotokea wakati wa kujifungua,” linasema gazeti Scientific American. “Vifo vya watoto wachanga vimepungua kwa asilimia 75 tangu mwaka wa 1960.” Lakini sayansi haijafanikiwa kurefusha maisha ya mwanadamu. “Hata baada ya utafiti wa miaka mingi, bado uzee ni fumbo kubwa,” linasema toleo lingine la Scientific American. Hata hivyo, “uthibitisho uliopo unaonyesha kwamba mwili huanza kuzeeka wakati ambapo maagizo katika chembe za urithi ambazo hudhibiti ukuzi huacha kufanya kazi vizuri.” Makala hiyo inaendelea kusema hivi: “Ikiwa kuzeeka kunasababishwa na utendaji wa chembe za urithi, inawezekana kwamba siku moja tatizo hilo litatatuliwa.”
“Hata baada ya utafiti wa miaka mingi, bado uzee ni fumbo kubwa”
Katika jitihada zao za kutafuta visababishi vya kuzeeka, kutia ndani magonjwa yanayohusiana na uzee, wanasayansi fulani wanachunguza maendeleo ya hivi karibuni katika elimu ya chembe za urithi inayoitwa epigenetics. Ni nini kinachohusika katika elimu ya epigenetics?
Kila chembe hai ina habari ambazo zinahitajika ili chembe mpya zifanyizwe. Nyingi ya habari hizo zinapatikana katika genome, yaani, mkusanyiko wa habari zote zilizo katika chembe za urithi. Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, wanasayansi wameanza kuchunguza kwa undani zaidi utendaji mbalimbali ndani ya chembe, yaani, kuchunguza epigenome, neno linalomaanisha kihalisi, “juu ya genome” yaani, jinsi habari iliyo ndani ya chembe za urithi itakavyotumika. Taaluma hiyo ya kuchunguza utendaji huo pamoja na utendaji wa kemikali zilizomo ndani ya chembe inaitwa epigenetics

Molekuli zinazofanyiza epigenome hazifanani hata kidogo na chembe za urithi. Chembe za urithi zinafanana na ngazi iliyojipinda, lakini epigenome ni alama au vibandiko vyenye kemikali ambavyo hujibandika juu ya chembe za urithi. Epigenome hufanya kazi gani? Kama kiongozi anavyoongoza kwaya, epiginome huelekeza jinsi habari zilizo kwenye chembe za urithi zitakavyotumiwa. Vibandiko hivyo vya molekuli hutendesha au kuzima chembe fulani za urithi kulingana na mahitaji ya chembe na mambo mengine yanayohusiana na mazingira ya mtu, kama vile aina ya vyakula anavyokula, mkazo anaokabili, na sumu anayopumua. Ugunduzi wa hivi karibuni kuhusu jinsi chembe za urithi zinavyoelekezwa umebadili sana maoni ya watu kuhusu sayansi ya biolojia ambayo inahusianisha utendaji wa chembe za urithi na magonjwa hususa na hata kuzeeka.
“Utendaji wa chembe za urithi umehusianishwa na magonjwa kama vile schizophrenia, baridi-yabisi, kansa, na maumivu ya kudumu,” anasema mtafiti wa utendaji wa chembe za urithi, Nessa Carey. Na “bila shaka unahusianishwa na uzee.” Kwa hiyo, uchunguzi wa utendaji wa chembe za urithi unaweza kutokeza matibabu yanayoweza kuboresha afya, kutibu magonjwa, kutia ndani kansa, na hivyo kurefusha maisha. Hata hivyo, kwa sasa, bado wanasayansi hawajafaulu. “Bado tunatumia mbinu za zamani [za kukabiliana na uzee],” anasema Carey, yaani “kula mboga nyingi” na “kufanya mazoezi mengi.”


Hata hivyo, kwa nini wanadamu wanajihangaisha sana kurefusha maisha yao? Kwa nini tunataka kuishi milele? Gazeti The Times la Uingereza liliuliza hivi: “Kwa nini wanadamu ulimwenguni pote wanahangaika sana kubuni njia za kuendelea kuishi, iwe ni kupata uhai usioweza kufa, ufufuo, kuendelea kuishi baada ya kifo, au kuzaliwa upya katika mwili mwingine?” Kama tutakavyoona, jibu la swali hilo linatusaidia kujua sababu hususa kwa nini tunazeeka.


Kwa Nini Tunataka Kuishi Milele?

Kwa maelfu ya miaka, watu wamejaribu kupata jibu la swali hilo. Je, kuna jibu linalopatana na akili, lenye kuridhisha na ambalo linaeleza kwa nini tuna tamaa ya kuishi milele? Je, tunaweza kujua kwa nini miili yetu ina uwezo wa kuishi milele? Mamilioni ya watu wangejibu kwa sauti kubwa, ndiyo! Kwa nini? Kwa sababu, walipojifunza Biblia walipata majibu yenye kuridhisha kuwahusu wanadamu.
Kuanzia mwanzo, Biblia inasema wazi kwamba ingawa wanadamu wanafanana kwa njia fulani na viumbe wengine, wao ni tofauti kabisa na viumbe hao. Kwa mfano, kwenye Mwanzo 1:27, tunasoma kwamba Mungu aliwaumba wanadamu kwa mfano wake. Jinsi gani? Alitupa uwezo wa kuonyesha upendo, haki, na hekima. Kwa kuwa Yeye anaishi milele, Mungu aliweka ndani yetu tamaa ya kuishi milele. “Ameweka umilele katika mioyo na akili ya wanadamu,” inasema Mhubiri 3:11.—The Amplified Bible.
Jambo moja katika mwili wa mwanadamu linaloonyesha kwamba wanadamu walikusudiwa waishi muda mrefu zaidi ya tunavyoishi ni uwezo wa ubongo, hasa uwezo wake wa kujifunza. Kitabu The Encyclopedia of the Brain and Brain Disorders (Kitabu Kuhusu Ubongo na Magonjwa ya Ubongo) kinasema kwamba kumbukumbu la muda mrefu la ubongo wa mwanadamu “halina kikomo.” Kwa nini ubongo uwe na uwezo huo mkubwa ikiwa haukukusudiwa kutumiwa? Kwa kweli, katika njia nyingi, miili yetu inaonyesha kusudi la Mungu la awali kwa wanadamu. Basi kwa nini tunazeeka, kuteseka, na kufa?
Kwa Nini Sisi Huzeeka na Kufa?

Mwanamume na mwanamke wa kwanza walikuwa na miili mikamilifu na pia walikuwa na uhuru wa kuchagua. Kwa kusikitisha, walitumia vibaya uhuru huo na kumwasi Muumba wao. * (Mwanzo 2:16, 17; 3:6-11) Kutotii kwao, au dhambi, kuliwafanya wahisi hatia kubwa na aibu. Pia kulifanya miili yao idhoofike na kuanza kufa polepole. “Mchomo unaotokeza kifo ni dhambi,” linasema andiko la 1 Wakorintho 15:56.
Kupatana na sheria ya asili ya urithi, wazao wote wa Adamu na Hawa walirithi kutokamilika, na pia mwelekeo wa kutenda dhambi, au wa kufanya yaliyo makosa. Andiko la Waroma 5:12 linasema hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”
Tufikie mkataa gani? Huu: Siri ya kuishi milele haitapatikana katika maabara. Ni Mungu tu anayeweza kurekebisha madhara yaliyosababishwa na dhambi. Lakini je, yeye atayarekebisha? Biblia inajibu kwa uhakika, ndiyo!

“Atameza Kifo Milele”

Tayari Mungu amechukua hatua kubwa ya kuondoa dhambi na kifo. Alimtuma Yesu Kristo ili afe kwa ajili yetu. Kifo cha Yesu kinawezaje kutusaidia? Yesu alizaliwa akiwa mkamilifu na “hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22) Kwa hiyo, yeye angeweza kuishi milele akiwa mwanadamu mkamilifu. Alifanya nini na uhai wake mkamilifu? Aliudhabihu ili kulipia dhambi zetu. Naam, Yesu alitoa uhai wake “kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Hivi karibuni, faida za fidia hiyo zitatumiwa kwa faida yetu. Hilo litamaanisha nini kwako? Fikiria maandiko haya.
“Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
“Yeye kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.
“Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26.
“Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.
Unaweza kuishi muda mrefu kadiri gani? Jibu la Biblia ni wazi: Wanadamu wanaweza kuwa na tumaini la kuishi milele—na tumaini hilo litatimizwa baada ya Mungu kuondoa uovu wote duniani. (Zaburi 37:28, 29) Yesu alikuwa na tumaini hilo lenye thamani akilini alipomwambia hivi mtu aliyetundikwa kando yake: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:43.
Tamaa ya wanadamu ya kuishi milele ni ya asili na itatimizwa. Mungu alituumba hivyo! Isitoshe, yeye atatosheleza tamaa hiyo. (Zaburi 145:16) Hata hivyo, ni lazima tutimize sehemu yetu. Kwa mfano, tunahitaji kuwa na imani katika Mungu. “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii,” linasema andiko la Waebrania 11:6. Hiyo si imani isiyo na msingi bali ni usadikisho unaotegemea ujuzi sahihi wa Biblia. (Waebrania 11:1)
Maelezo ya Chini^ fu. 21 Uasi wa Adamu na Hawa ulitokeza masuala mazito ya kiadili yaliyomhusisha Mungu. Masuala hayo ambayo yanaonyesha ni kwa nini Mungu amevumilia uovu kwa muda, yanazungumziwa katika kitabu cha kujifunzia Biblia, Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Je, Unaweza Kuishi Maisha Marefu Ukiwa na Afya Hata Sasa?

Katika uchunguzi uliofanywa kwa mara ya kwanza uliohusisha watu zaidi ya 1,500 waliozaliwa karibu na mwaka wa 1910, wanasayansi wa mambo yanayohusiana na afya, Howard S. Friedman na Leslie R. Martin walidai kwamba mambo yanayoweza kuonyesha ikiwa mtu ataishi muda mrefu ni umakini na kuwa na marafiki wengi. Friedman na Martin walisema, “Watu walio makini hufanya mambo mengi ili kulinda afya yao na hawajihusishi katika utendaji utakaohatarisha uhai wao. Yaelekea hawatavuta sigara, kunywa kileo kupita kiasi, kutumia dawa za kulevya, au kuendesha gari kwa kasi sana. Wana mwelekeo wa kufunga mkanda wa usalama na kufuata maagizo ya daktari. Si kwamba hawataki kujasiria kufanya mambo hatari bali wao hujitahidi kutovuka mipaka.”
Kuhusu marafiki, watu walioishi kwa muda mrefu “walikuwa na marafiki wengi na . . . waliwasaidia wengine.” Waandishi hao wanasema kwamba sayansi huthibitisha ule msemo unaosema, “Wema hawana maisha, wabaya huishi muda mrefu” ni uwongo. “Kwa ujumla . . . wabaya hufa mapema, na wema huishi muda mrefu.”

No comments:

Leave a Reply