Latest News


More

NGONO KABLA YA NDOA: Je ni vibaya kufanya Ngono kabla ya ndoa?

Posted by : Unknown on : Monday, August 19, 2013 0 comments
Unknown
Saved under :

“Kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, . . . kwamba mjiepushe na uasherati.”—1 Wathesalonike 4:3.

WATU HUSEMA NINI?

Tamaduni fulani huruhusu matendo ya ngono kati ya watu wazima ambao hawajafunga ndoa ikiwa watu hao wanakubaliana. Katika maeneo fulani, vijana ambao hawajaoana wanaruhusiwa kushiriki katika aina fulani za mahusiano ya ngono.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inatumia neno “uasherati” kufafanua baadhi ya matendo ya ngono yanayofanywa nje ya ndoa. Mungu anawatazamia waabudu wake ‘wajiepushe na uasherati.’ (1 Wathesalonike 4:3) Uasherati unaorodheshwa kati ya dhambi nzito pamoja na uzinzi, kuwasiliana na pepo, ulevi, kuabudu sanamu, kuua, na wizi.—1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Sababu moja ni kwamba Biblia inaonya kuwa “Mungu atawahukumu waasherati.” (Waebrania 13:4) Zaidi ya hilo, tukitii sheria za Mungu kuhusu maadili ya ngono, tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova Mungu. (1 Yohana 5:3) Yeye naye huwabariki wale wanaoshika amri zake.—Isaya 48:18.

Je, ni vibaya kwa watu wawili ambao hawajafunga ndoa kushiriki matendo fulani ya ngono?

“Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu.”—Waefeso 5:3.

WATU HUSEMA NINI?

Watu wengi husema kwamba maadamu hawafanyi ngono, hakuna ubaya wowote kwa watu wawili ambao hawajafunga ndoa kushiriki katika matendo mengine ya ngono.

BIBILIA INASEMA NINI?

Inapozungumzia matendo ya ngono yasiyo ya adili, Biblia haitaji tu uasherati bali pia inataja “unajisi,” au uchafu wa kingono na “mwenendo mpotovu.” (2 Wakorintho 12:21) Ni wazi kwamba kuna matendo fulani ya kingono yanayomchukiza Mungu yanapofanywa nje ya ndoa hata kama hayahusishi kufanya ngono.

Kwa ujumla, maoni ya Biblia kuhusu ngono ni kwamba mahusiano ya kingono yanapaswa kuwa tu kati ya mwanamume na mwanamke waliooana. Biblia inakataza pia “hamu yenye tamaa ya ngono.” (1 Wathesalonike 4:5) Hilo linamaanisha nini? Fikiria mfano huu ambao unaweza kuwahusu wanaume na wanawake pia: Huenda mwanamke akaazimia kwamba hatafanya ngono na mpenzi wake. Hata hivyo, anajihusisha katika mahusiano mengine ya kingono na mpenzi wake. Kwa kufanya hivyo, wanatamani au wana uchu kuelekea kitu ambacho si chao. Kwa hiyo, wana hatia ya kuwa na “hamu yenye tamaa ya ngono.” Biblia inashutumu aina hiyo ya pupa ya ngono.—Waefeso 5:3-5.

Unaweza kujiepushaje na ukosefu wa maadili katika ngono?

“Ukimbieni uasherati.”—1 Wakorintho 6:18.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Biblia inasema kwamba watu wanaofanya ngono kabla ya kufunga ndoa wanahatarisha urafiki wao pamoja na Mungu.—Wakolosai 3:5, 6.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inawashauri watu ‘waukimbie uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18) Hilo linamaanisha kwamba mtu anapaswa kukaa mbali kabisa na kitu chochote kinachoweza kumshawishi afanye uasherati. (Methali 22:3) Kwa mfano, ili mtu abaki akiwa safi kiadili, ni muhimu aepuke kushirikiana kwa ukaribu na watu ambao hupuuza kanuni za Mungu kuhusu ngono. Biblia inaonya hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

Pia, mtu akilisha akili yake mambo yasiyo ya adili, anaweza kutumbukia katika mwenendo mpotovu kingono. (Waroma 8:5, 6) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuepuka muziki, video, machapisho, na jambo lolote ambalo linaonyesha matendo yasiyofaa ya ngono au mwenendo wa kingono unaomchukiza Mungu.—Zaburi 101:3.

No comments:

Leave a Reply