Latest News


More

YESU KRISTO NI NANI? ...ALITOKA WAPI?

Posted by : Unknown on : Thursday, August 22, 2013 0 comments
Unknown
Saved under :

1. Yesu alitoka wapi?


Tofauti na mwanadamu mwingine yeyote, Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho kabla ya kuzaliwa hapa duniani. (Yohana 8:23) Alikuwa kiumbe wa kwanza kuumbwa na Mungu, naye alisaidia kuumba vitu vingine vyote. Anaitwa Mwana “mzaliwa-pekee” wa Mungu kwa kuwa yeye pekee ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Yehova. (Yohana 1:14) Yesu pia anaitwa “Neno” kwa kuwa alikuwa msemaji wa Mungu.—Soma Methali 8:22, 23, 30; Wakolosai 1:15, 16.
2. Kwa nini Yesu alikuja duniani?

Mungu alimtuma Mwana wake duniani kwa kuuhamisha uhai wake kutoka mbinguni na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira Myahudi aliyeitwa Maria. Kwa hiyo Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu. (Luka 1:30-35) Yesu alikuja duniani (1) kufundisha ukweli kumhusu Mungu, (2) kutuwekea mfano wa jinsi tunavyoweza kufanya mapenzi ya Mungu hata tukiwa katika hali ngumu, na (3) kuutoa uhai wake mkamilifu uwe “fidia.”—Soma Mathayo 20:28.
3. Kwa nini tunahitaji fidia?
Fidia ni kitu kinachotolewa kama malipo ili kumkomboa mtu anayekabili kifo. (Kutoka 21:29, 30) Mungu hakukusudia wanadamu wazeeke na kufa. Tunajuaje jambo hilo? Mungu alimwambia mwanadamu wa kwanza, Adamu, kuwa iwapo angefanya kile ambacho Biblia hukiita “dhambi,” angekufa. Kama Adamu hangefanya dhambi, hangekufa. (Mwanzo 2:16, 17; 5:5) Kulingana na Biblia, kifo ‘kiliingia’ ulimwenguni kupitia Adamu. Hivyo, Adamu aliwapitishia wazao wake wote dhambi pamoja na adhabu ya dhambi, yaani, kifo. Tunahitaji fidia ili tukombolewe kutoka katika adhabu ya kifo tuliyorithi kutoka kwa Adamu.—Soma Waroma 5:12; 6:23.
Ni nani ambaye angeweza kulipa fidia ili kutukomboa kutoka katika kifo? Tunapokufa, tunalipia adhabu ya dhambi zetu tu. Mwanadamu ambaye si mkamilifu hawezi kulipia dhambi za wengine.—Soma Zaburi 49:7-9.
4. Kwa nini Yesu alikufa?

Tofauti nasi, Yesu alikuwa mkamilifu. Kwa hiyo hakuhitaji kufa kwa ajili ya dhambi zake kwa sababu hakuwahi kutenda dhambi yoyote. Badala yake, Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi za wengine. Mungu alimtuma Mwana wake afe kwa ajili yetu ili kuonyesha upendo Wake mkubwa kwa wanadamu. Yesu pia alituonyesha upendo kwa kumtii Baba yake na kuutoa uhai wake kwa ajili ya dhambi zetu.—Soma Yohana 3:16; Waroma 5:18, 19.
5. Yesu anafanya nini sasa?

Alipokuwa duniani, Yesu aliwaponya wagonjwa, aliwafufua wafu, na kuwasaidia watu waliokuwa katika taabu. Hivyo, alionyesha mambo atakayowafanyia wanadamu watiifu wakati ujao. (Mathayo 15:30, 31; Yohana 5:28) Baada ya Yesu kufa, Mungu alimfufua akiwa kiumbe wa roho. (1 Petro 3:18) Kisha, Yesu akangoja akiwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu mpaka alipopewa mamlaka ya kutawala akiwa Mfalme juu ya dunia yote. (Waebrania 10:12, 13) Sasa Yesu anatawala akiwa Mfalme mbinguni, na wafuasi wake wanatangaza habari hiyo njema duniani kote.—Soma Danieli 7:13, 14; Mathayo 24:14.
Karibuni, Yesu atatumia mamlaka yake akiwa Mfalme kukomesha mateso yote na wale wanaoyasababisha. Wote wanaomwamini Yesu na kumtii watafurahia uhai katika dunia paradiso.—Soma Zaburi 37:9-11.

No comments:

Leave a Reply