Latest News


More

WANAFUNZI WA DARASA LA SABA WAANZA MITIHANI YAO YA KUMALIZA SHULE LEO

Posted by : Unknown on : Wednesday, September 11, 2013 0 comments
Unknown
Saved under :


WANAFUNZI 868,030 wanatarajiwa kufanya mtihani wakumaliza elimu ya msingi na maandalizi yamekamilika.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, NaibuWaziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Bw.Philipo Mulugo, alisema mtihani huo unatarajiwa kuanza leo. Kati ya wanafunzi wanaotarajiwa kufanya mtihani huo , wavulana ni 412,105 sawa na asilimia 47%, wasichana ni 445,925 sawa na asilimia 52% .

Alitoa wito kwa Maofisa Elimu katika mikoa na Halmashauri kuhakikisha taratibu zote za mitihani zinazingatiwa pamoja na kuandaa mazingira salama yatakayozuia mianya inayoweza kusababisha udanganyifu.“Nawaonya wasimamizi wote, wawe makini na waadilifu katika kipindi chote cha mitihani, kujiepusha na vitendo vya udanganyifu kwani Serikali haitasita kumchukulia hatua kali za kisheria mtu yeyote atakayekiuka taratibu zilizopo,” alisema.

Aliwataka wanafunzi wote kuzingatia taratibu za mitihani ili matokeo yao yaoneshe uwezo wao halisi kulingana na maarifa waliyoyapata wakiwa shuleni kwa kujiepushe na vitendo vya udanganyifu ili kuepuka kufutiwa mitihani yao. Alisema wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao pembezoni mwa shule hizo, waondoke katika maeneo hayo ili kuwapa nafasi nzuri wanafunzi kufanya mitihani yao kwa utulivu zaidi.

Akizungumzia mfumo wa usahihishaji Bw. Mulugo alisema umeonesha mafanikio makubwa katika mitihani iliyopita kwani karatasi zote zilipita katika mashine maalumu bila matatizo. Aliongeza kuwa, Serikali imetenga sh. milioni 400 kwa ajili ya kuandaa vyeti ambavyo vinamfanya mwanafunzi atambulike kama mhitimu wa elimu ya msingi.

“Fedha hizi zimetengwa na Serikali, mzazi yeyote haruhusiwi kuchangia, kama yupo ambaye atatozwa fedha atujulishe,” alisema. Awali, Bw. Mulugo alisema kati ya malengo tisa ya mpango ya matokeo makubwa sasa (Big results now), kwa upande wa sekta ya elimu Serikali ipo katika mkakati wa kuhakikisha wanafunzi wa darasa la pili watapewa mtihani ili kutambua uwezo wao wa kujua kusoma, kuandika kabla ya kuendelea darasa tatu.

No comments:

Leave a Reply