Huenda usifaulu kabisa kuwazuia watu kueneza
porojo kukuhusu, hata hivyo unaweza kuchagua jinsi utakavyoitikia
ukigundua kwamba mtu fulani ameeneza porojo kukuhusu. Ukigundua kwamba habari
fulani kukuhusu imeenea, kuna angalau mambo mawili unayoweza kufanya.
JAMBO LA 1: Puuza. Mara
nyingi kupuuza jambo fulani ndio uamuzi bora kabisa
—hasa ikiwa habari
zilizoenezwa ni za upuuzi. Fuata ushauri huu wa Biblia: “Usiwe na haraka
kuudhika katika roho yako.”—Mhubiri 7:9.
“Habari zilienea kuwa nilikuwa
nikimchumbia mvulana fulani—mtu ambaye hata sikuwahi kukutana naye! Ulikuwa
upuuzi mtupu na kwa hiyo niliamua kuupuza.”—Elise.
“Ukiwa na sifa nzuri ni rahisi kwako
kukabiliana na porojo. Hata habari mbaya zikienezwa kukuhusu, ni watu wachache
watakaoziamini, kwa sababu wanajua kwamba una sifa nzuri. Zitakusaidia uendelee
kudumisha hadhi yako.”—Allison.
Dokezo: Andika (1) jambo
ambalo lilienezwa kukuhusu na (2) jinsi ulivyohisi. ‘Ukishasema moyoni mwako,’
huenda ukatambua kwamba ni rahisi zaidi kuamua kulipuuza au kulisahau jambo
hilo.
—Zaburi 4:4.
JAMBO LA 2: Mfikie mtu aliyeanzisha
porojo hiyo. Katika visa fulani huenda ukahisi kwamba habari mbaya sana
kukuhusu imeenezwa hivi kwamba ukaamua kuchukua hatua ya kumfikia yule
aliyeianzisha.
“Unapowafikia watu wanaoeneza porojo
kukuhusu, huenda ukawasaidia watambue kwamba hatimaye mambo wanayosema humfikia
mtu wanayeeneza habari zake. Hilo huenda likakusaidia ujisafishie jina au hata
kusuluhisha tatizo lenyewe.”—Elise.
Kabla ya kumfikia mtu anayeeneza porojo
kukuhusu, fikiria kanuni zifuatazo za Biblia na ujiulize maswali
yaliyoambatanishwa na kanuni hizo.
-
“Yeyote anapojibu jambo kabla ya
kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (
Methali 18:13) ‘Je, nina habari zote
zinazohusika? Je, inawezekana kwamba mtu aliyeniletea porojo hizo hakuelewa
vizuri mambo aliyosikia?’
-
‘Uwe mwepesi wa kusikia, si mwepesi
wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (
Yakobo 1:19) ‘Je, huu ndio wakati
unaofaa wa kumfikia mtu anayeeneza porojo kunihusu? Je, nina uhakika kwamba
ninatumia njia inayofaa kusuluhisha jambo hilo? Au ni afadhali zaidi nisubiri
wakati fulani upite ili hisia zangu zitulie?’
-
“Chochote ambacho mngetaka mtendewe
na watu, ninyi nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (
Mathayo 7:12,
Holy Bible)
‘Ikiwa ningekuwa nimeeneza porojo kumhusu mtu mwingine, ningetaka mtu huyo
anifikie kwa njia gani? Ningependa tuzungumzie tatizo hilo chini ya hali gani?
Ningependa atumie maneno ya aina gani na azungumze kwa njia gani?’
Dokezo: Kabla ya kumfikia
yule anayeeneza porojo kukuhusu, andika mambo utakayomwambia. Kisha subiri juma
moja au mawili, halafu urudie mambo uliyoandika uone kama kuna mabadiliko yoyote
unayohitaji kufanya. Kisha zungumzia mambo hayo na mzazi wako au rafiki mkomavu
na umwombe mashauri.
Ukweli wa mambo: Kama
ilivyo na mambo mengi maishani, huwezi kuwazuia watu wasieneze porojo. Lakini
hilo halimaanishi kwamba ni lazima porojo ikudhibiti!
(Source:www.jw.org)
No comments: