Ikiwa wewe na mwenzi wako hamwelewani inapohusu jinsi ya kushughulika na wakwe, jitahidini kurekebisha tatizo hilo kwa pamoja. Fuateni ushauri huu wa Biblia: ‘Tafuteni amani, na kuifuatia.’—
Zaburi 34:14.
Ili kufanya hivyo, fikiria hali zifuatazo. Kila hali inaonyesha mtazamo wa mume au mke. Hata hivyo, wote wawili wanakabili changamoto zilezile na kanuni zitakazoonyeshwa zinaweza kuwasaidia kushughulika na wakwe.
Mke wako anasema kwamba angefurahi ikiwa ungekuwa na uhusiano mzuri na mama yake. Lakini unaona ni vigumu kushughulika na mama yake.
Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mke wako kuhusu tatizo hilo na uwe tayari kufanya marekebisho. Jambo kuu si namna unavyohisi kuhusu mama-mkwe bali jinsi unavyohisi kuhusu mwenzi wako uliyeapa kwamba utampenda. Wakati wa mazungumzo mwambie njia moja au mbili hususa utakazotumia kuboresha uhusiano wako na mama yake na ujitahidi kufanya hivyo. Kadiri anavyoona jitihada zako, mke wako atakuheshimu zaidi.
—Kanuni ya Biblia: 1 Wakorintho 10:24.
Mume wako anasema kwamba unawahangaikia zaidi wazazi wako kuliko yeye.
Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mume wako kuhusu tatizo hilo ili kujua maoni yake. Ni kweli kwamba mume wako hahitaji kuwa na hofu ya namna hiyo ikiwa unawaheshimu wazazi wako. (
Methali 23:22) Hata hivyo, unahitaji kumhakikishia kupitia maneno na matendo yako kwamba bado unamthamini sana. Akiwa na uhakika huo, mume wako hatahisi kwamba anashindana na wazazi wako ili tu umthamini.
—Kanuni ya Biblia: Waefeso 5:33.
Mke wako anaomba ushauri kwa wazazi wake badala ya kukuomba wewe.
Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mke wako na mkubaliane kuhusu mambo ambayo mnaweza kuomba ushauri wa wazazi. Jitahidi kuwa mwenye kukubali sababu. Je,
mara zote ni vibaya kuongea na mzazi kuhusu tatizo fulani? Ni wakati gani unaofaa wa kuzungumza nao? Mkikubaliana kuweka mipaka yenye usawaziko, hali hiyo haitakuwa tatizo.
—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 4:5.
No comments: