Latest News


More

Banza Tshikala: Kutoka Soka hadi Mchungaji Kanisani

Posted by : Unknown on : Monday, May 13, 2013 0 comments
Unknown
Saved under : ,
Ni jioni tulivu nipo maeneo ya Sinza jijini Dar es Salaam, namwona mtu ninayeamini namfahamu, lakini sikumbuki ni nani. Hata hivyo kutokana na uzoefu nilionao kwenye mambo ya mpira, nahisi ni mchezaji ingawa bado nashindwa kumkumbuka.

Natamani kumjua ni nani namfuatilia, mbele kidogo maeneo ya Sinza Legho, anaingia mtaa upande wa kulia wa barabara. Licha ya safari yangu kuwa inaishia hapo, lakini nililazimika kumfuatilia na kabla ya kukata shauri la kumsimamisha na kumuuliza namkumbuka kuwa, si mwingine bali ni aliyewahi kuwa mchezaji wa timu ya Yanga Banza Tshikala.

Nikimwangalia anaonekana ni mwenye siha njema, namkimbilia ili niseme naye mawili, matatu. Msomaji usishangae kwa nini namfuatilia, hii ni kutokana na kupenda michezo hasa kwa wachezaji wa zamani waliofanya maajabu wakiwa katika soka’.

Kwa mshangao natokea katika kanisa kubwa ambapo Banza anaingia ndani yake. Kutokana na kutokuwa na mavazi yanayoniruhusu kuwepo eneo hilo naondoka bila kutimiza lengo langu.

Nakutana na Mhariri wangu wa magazeti ya mwisho wa juma Julius Magodi na kumfahamisha kuhusu kukutana na mchezaji huyo, ananipatia usafiri na kunitaka nimfuatilie siku inayofuata ambayo ni Jumapili.

Nafanya hivyo na kwa bahati nzuri wakati nafika kanisani hapo na kumkuta Banza akimwombea binti ambaye bila shaka alikuwa na matatizo. Nasubiri hadi misa ya maombezi inaisha, nakutana rasmi na mchezaji huyo aliyewahi kuichezea Yanga kwa misimu mitano. Nasalimiana naye na mwisho wa yote najitambulisha kwake, naye bila hiyana ananikaribisha ofisini kwake.

Nakutana na mchungaji mkuu wa kanisa hilo linaloitwa The Oasis Of Hearling Minitries, Prosper Ntepa na kupewa baraka zote za kufanya mahojiano na Banza ambaye ni mchungaji wa vijana katika kanisa hilo.

Banza anaanza kuelezea historia yake ya maisha kuwa alizaliwa Julai 27 mwaka 1972, nchini Kongo.

Kwa ufupi anaeleza safari yake ya kucheza soka katika ardhi ya Tanzania kuwa iliianza mwaka 1994, alipokuja na timu ya TP Mazembe akiwa ni mchezaji kwenye timu hiyo akicheza namba nne na sita, ambapo walikuwa na mechi za kirafiki na timu za Simba ,Yanga, Pan African na Tukuyu Stars.

Anasema kuwa katika mechi hizo za kirafiki walifanikiwa kuifunga Simba bao 1-0, Tukuyu Stars bao 2-0 na Pan Afrika mabao 2-0 na kufungwa na Yanga bao 1-0.

Anabainisha kuwa katika mechi hizo za kirafiki ndipo alipoonwa na viongozi wa timu ya Tukuyu Stars wakatuma watu Kongo kwa ajili ya kumsajili.

“Viongozi wa Tukuyu ndiyo walikuja Kongo na nikafanya nao mazungumzo tukakubaliana, nikasajiliwa kwenye timu hiyo kwa mkataba wa miaka miwili huku nikipewa Dola za Marekani 500 (Sh800,000 za sasa), ili nimalizie mambo yangu. Mkataba ulikuwa ni kiasi cha Dola300 (Sh480,000) kila mwezi ambapo kocha alikuwa Juma Athumani na Mwenge Yavu, huku mfadhili akiitwa ‘kaka’ namfahamu kwa jina moja,”anasema Tshikala.
(Habari na Kalunde Jamal wa Mwananchi Communication)

No comments:

Leave a Reply