Latest News


More

BIBLIA INASEMA NINI KUHUSU KUWA JEURI

Posted by : Unknown on : Thursday, April 23, 2015 0 comments
Unknown
Saved under :


Historia ya wanadamu imejaa jeuri. Je, hali hiyo yenye kuhuzunisha itaendelea milele?

Mungu ana maoni gani kuhusu jeuri?

WATU WANASEMA NINI?

Watu wengi, kutia ndani wanadini, wanaona kwamba inafaa kutenda kwa jeuri unapochokozwa. Mamilioni ya watu huona kwamba jeuri inayoonyeshwa kwenye vyombo vya habari ni burudani inayofaa.

BIBLIA INASEMA NINI?

Karibu na eneo la mji wa Mosul, kaskazini mwa Iraki, kuna mabomoko ya jiji la Ninawi, lililokuwa mji mkuu wa Milki ya kale ya Ashuru. Jiji hilo lilipokuwa linazidi kusitawi, Biblia ilitabiri kwamba Mungu “atafanya Ninawi kuwa mahame yenye ukiwa.” (Sefania 2:13) Mungu alisema hivi: “Nami nitakuweka uwe tamasha.” Kwa nini? Kwa sababu Ninawi lilikuwa “jiji la umwagaji wa damu.” (Nahumu 1:1; 3:1, 6) Andiko la Zaburi 5:6 linasema kwamba, “Mtu anayemwaga damu . . . Yehova anamchukia.” Mabomoko ya Ninawi yanaonyesha wazi kwamba Mungu alitenda kulingana na unabii wake.
Jeuri ilianzishwa na adui mkuu wa Mungu na wanadamu—Shetani Ibilisi, ambaye Yesu Kristo alimwita “muuaji.” (Yohana 8:44) Pia, kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” tabia zake zinaonyeshwa wazi kupitia maoni ya watu kuhusu jeuri, kutia ndani ulimwengu kupenda matendo ya jeuri yanayoonyeshwa kwenye vyombo vya habari. (1 Yohana 5:19) Ili kumpendeza Mungu, tunapaswa kuchukia jeuri na kupenda yale ambayo Mungu anapenda. * Je, hilo linawezekana?
“Yehova . . . na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.”Zaburi 11:5.

Je, watu wenye jeuri wanaweza kubadilika?

WATU WANASEMA NINI?

Jeuri ni tabia ya asili ya mwanadamu isiyoweza kubadilika.

BIBLIA INASEMA NINI?

Ondoleeni mbali “ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu.” Pia inasema hivi: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya.” (Wakolosai 3:8-10) Je, Mungu anadai mengi mno kwa kutaka tufanye hivyo? Hapana. Watu wanaweza kubadilika. * Jinsi gani?
Hatua ya kwanza ni kupata ujuzi sahihi kuhusu Mungu. (Wakolosai 3: 10) Mtu mwenye moyo mnyofu anapojifunza kuhusu sifa  na viwango vinavyovutia vya Muumba wetu, anamkaribia Mungu kwa sababu anampenda na anataka kumpendeza.—1 Yohana 5:3.
Hatua ya pili inahusu watu tunaoamua kushirikiana nao. “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu, ili usizoee njia yake na hakika uiwekee nafsi yako mtego.”—Methali 22:24, 25.
Hatua ya tatu inahusu utambuzi. Tambua kwamba jeuri ni udhaifu mkubwa unaoonyesha kwamba mtu amekosa sifa ya kujizuia. Hata hivyo, mtu mwenye kufanya amani anaonyesha utambuzi. Andiko la Methali 16:32 linasema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu.”
“Fuatilieni amani pamoja na watu wote.”Waebrania 12:14.

Je, jeuri itakwisha?

WATU WANASEMA NINI?

Sikuzote kumekuwa na jeuri, nayo haitakwisha.

BIBLIA INASEMA NINI?

“Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Hivyo, ili kuwaokoa wapole na wenye kufanya amani, Mungu atawaangamiza wale wanaopenda jeuri kama alivyofanya katika jiji la kale la Ninawi. Kisha, dunia haitakuwa tena na jeuri.—Zaburi 72:7.
Mwanamke akipanda maua katika mazingira yenye amani
“Wale walio na tabia-pole . . . watairithi dunia.”—Mathayo 5:5
Kwa hiyo, sasa ni wakati wa kutafuta kibali cha Mungu kwa kusitawisha mtazamo wa kufanya amani. Andiko la 2 Petro 3:9 linasema hivi: “Yehova . . . ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”
“Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu.”Isaya 2:4.

(Source: www.jw.org) 

No comments:

Leave a Reply