Latest News


More

JE BIBLIA INAKUBALI UBASHIRI WA KUTUMIA NAMBA?

Posted by : Unknown on : Thursday, April 23, 2015 0 comments
Unknown
Saved under :


Jibu La Biblia

Katika Biblia, mara nyingi namba hutumiwa kwa kihalisi, hata hivyo nyakati nyingine hutumiwa kwa njia ya mfano. Muktadha wa andiko unaweza kutusaidia kujua ikiwa namba fulani inatumiwa kwa njia ya mfano au la. Fikiria baadhi ya namba ambazo zinatumiwa kwa njia ya mfano katika Biblia:
  • 1 Umoja au muungano. Kwa mfano, Yesu alimwomba Mungu kwamba wafuasi wake “wote wapate kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo katika muungano pamoja na wewe.”Yohana 17:21; Mathayo 19:6.
  • 2 Katika mambo ya kisheria, mashahidi wawili huthibitisha ukweli wa jambo fulani. (Kumbukumbu la Torati 17:6) Vivyo hivyo, kurudia maono au maneno fulani kulihakikisha kwamba jambo hilo lilikuwa hakika na la kweli. Kwa mfano, Yosefu alipokuwa akifasiri ndoto ya Farao wa Misri, alisema hivi: “Kwa kuwa ndoto hiyo ilirudiwa mara mbili kwa Farao inamaanisha kwamba jambo hilo limewekwa imara na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 41:32) Katika unabii, “pembe mbili” zinaweza kuwakilisha serikali pacha, kama vile nabii Danieli alivyoambiwa kuhusu Milki ya Umedi na Uajemi.Danieli 8:20, 21; Ufunuo 13:11.
  • 3 Sawa na vile mashahidi watatu wanavyoweza kuhakikisha kabisa jambo fulani kuwa la kweli, kurudia jambo mara tatu kunakazia au kuonyesha kwamba linalosemwa ni hakika.Ezekieli 21:27; Matendo 10:9-16; Ufunuo 4:8; 8:13.
  • 4 Namba hii inaweza kumaanisha ukamili katika umbo au katika utendaji, kama vile katika maneno “pembe nne za dunia.”Ufunuo 7:1; Isaya 11:12; Ufunuo 21:16.
  • 6 Kwa kuwa namba hii imepungua saba inayowakilisha ukamilifu, sita inasimamia kutokamilika au lisilo kamilifu, au jambo linalohusianishwa na maadui wa Mungu.1 Mambo ya Nyakati 20:6; Danieli 3:1; Ufunuo 13:18.
  • 7 Namba hii hutumiwa mara nyingi kumaanisha ukamilifu. Kwa mfano, Waisraeli waliagizwa na Mungu kuzunguka jiji la Yeriko kwa siku saba, na kuizunguka mara saba katika siku ya mwisho. (Yoshua 6:15) Biblia ina mifano mingi ambapo namba saba imetumiwa kwa njia hiyohiyo. (Mambo ya Walawi 4:6; 25:8; 26:18; Zaburi 119:164; Ufunuo 1:20; 13:1; 17:10) Yesu alipomwambia Petro kwamba amsamehe ndugu yake “si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77,” kurudia namba 7 kulionyesha kwamba alipaswa kuendelea kusamehe “bila kuacha”.Mathayo 18:21, 22.
  • 10 Namba hii inaweza kuwakilisha jumla ya kitu, au kukusanya pamoja.Kutoka 34:28; Luka 19:13; Ufunuo 2:10.
  • 12 Namba hii inaweza kumaanisha ukamili kuhusiana na kusudi la Mungu. Kwa mfano, mtume Yohana alipewa maono ya kimbingu ambapo aliona jiji lililokuwa na “mawe ya msingi kumi na mawili, na juu ya hayo majina kumi na mawili ya mitume.” (Ufunuo 21:14; Mwanzo 49:28) Namba 12 ikizidishwa mara kadhaa pia inaweza kuwa na maana hiyohiyo.Ufunuo 4:4; 7:4-8.
  • 40 Baadhi ya hukumu au adhabu ilihusianishwa na namba 40.Mwanzo 7:4; Ezekieli 29:11, 12.

Ubashiri kwa kutumia namba

Jinsi ambavyo namba imetumiwa kwa njia ya mfano katika Biblia ni tofauti na jinsi inavyotumiwa katika kubashiri. Watu wengine hufanya uchawi kwa kutumia namba, kupatanisha namba, na kujumlisha namba mbalimbali ili kubashiri matukio. Kwa mfano, kikundi fulani cha Wayahudi kimechunguza maana zilizofichika kwenye Maandiko ya Kiebrania kwa kutumia njia inayoitwa gematria, ambayo inahusisha kutafuta namba fulani ya siri katika namba zinazolingana kwenye herufi. Ubashiri wa kutumia namba ni namna ya uaguzi, tendo ambalo Mungu anakataza.Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

No comments:

Leave a Reply