Latest News


More

JINSI YA KUMWEKEA KIJANA WAKO SHERIA

Posted by : Unknown on : Thursday, April 23, 2015 0 comments
Unknown
Saved under :




KIKWAZO

Kijana wako anasema wewe ni mkali sana. Hata hivyo, kwa sababu ya tamaa yako ya kiasili ya kumlinda unajiambia hivi, ‘Ikiwa nitalegeza sheria kijana wangu ataingia matatani!’
Unaweza kumwekea kijana wako sheria zenye usawaziko. Lakini kwanza unahitaji kujua ni nini kinachomfanya akasirishwe na sheria unazoweka.

KWA NINI HILI HUTUKIA

Dhana: Matineja wote huasi sheria; ni jambo lisiloepukika wakati wa ujana.
Jambo Hakika: Huenda tineja asiasi ikiwa wazazi wataweka sheria zenye usawaziko na kuzizungumzia pamoja naye.
Ingawa kuna mambo mengi yanayoweza kuchangia tineja kuasi, huenda wazazi bila kujua wakachochea jambo hilo ikiwa watashikilia sana sheria au wataweka sheria ambazo hazifai umri wa tineja. Fikiria mambo yafuatayo:
  • Kushikilia sana sheria. Wazazi wanapoweka sheria bila kuizungumzia pamoja na kijana wao, sheria hiyo inakuwa kama pingu inayombana badala ya kuwa mkanda wa usalama unaomlinda. Tokeo ni kwamba, huenda tineja akafanya kisiri mambo yaleyale ambayo wazazi wake wanamkataza.
  • Sheria ambazo hazifai umri wa tineja. “Kwa sababu nimesema,” jibu hilo linaweza kumridhisha mtoto mdogo, lakini vijana wanaobalehe wanahitaji maelezo zaidi—wanahitaji sababu. Isitoshe, hivi karibuni, kijana wako ataishi peke yake na atahitaji kujifanyia mwenyewe maamuzi muhimu. Kwa hiyo ni jambo linalofaa kwake ajifunze kufikiri vizuri na kufanya maamuzi mazuri sasa, wakati bado yupo chini ya uangalizi wako.
Lakini unaweza kufanya nini ikiwa inaonekana kwamba daima kijana wako hukasirishwa na sheria zako?

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Kwanza, tambua kwamba matineja wanahitaji—na hata wanataka sanakuwekewa mipaka. Kwa hiyo weka sheria, na uhakikishe kwamba kijana wako anazielewa. Kitabu Letting Go With Love and Confidence kinasema hivi, “Vijana wanaobalehe wanapowekewa mipaka iliyo wazi na kutazamia wazazi wawape mwongozo fulani, ni vigumu kwao kujiingiza katika tabia zisizofaa.” Kinyume cha hilo, wazazi ambao huhisi kwamba hakuna uhitaji wa kuweka sheria huwafanya vijana wao wafikiri kwamba wazazi wao hawajali. Na kwa hakika jambo hilo huwafanya waasi.—Kanuni ya Biblia: Methali 29:15.
Unawezaje kuonyesha usawaziko? Acha kijana wako aeleze anavyohisi kuhusu sheria za familia. Kwa mfano, ikiwa anaomba muda aliyowekewa wa kurudi nyumbani urekebishwe, msikilize anapoeleza sababu zake. Huenda ikawa rahisi zaidi kwa tineja kuheshimu na kufuata maamuzi unayofanya—hata kama hakubaliani nayo—ikiwa anahisi kwamba umemsikiliza kwa makini.— Kanuni ya Biblia: Yakobo 1:19.
Hata hivyo, kabla ya kufanya maamuzi kumbuka jambo hili: Matineja huwa na mwelekeo wa kutaka uhuru zaidi kuliko wanavyostahili, na wakati huohuo wazazi huenda wakawa na mwelekeo wa kuwapa matineja uhuru kidogo kuliko wanavyopaswa kuwapa. Kwa hiyo, fikiria kwa uzito ombi la kijana wako. Je, ameonyesha kuwa anaweza kutegemeka? Je, sheria inaweza kubadilishwa kwa sababu ya hali? Inapofaa, uwe tayari kubadilikana kulingana na hali.—Kanuni ya Biblia: Mwanzo 19:17-22.
Mbali na kusikiliza hisia za kijana wako, hakikisha pia yeye anajua mahangaiko yako kumhusu. Kwa kufanya hivyo, unamfundisha kutofikiria mapendezi yake tu bali pia afikirie hisia za wengine.—Kanuni ya Biblia: 1 Wakorintho 10:24.
Mwishowe, fanya uamuzi na ueleze sababu za uamuzi huo. Hata kama hapendezwi na uamuzi huo, yaelekea atafurahi kuwa na wazazi wanaomsikiliza na kutaka kujua maoni yake. Kumbuka, unamfundisha kijana wako anayebalehe kutenda kama mtu mzima. Kwa kumwekea kijana wako sheria zinazofaa na kuzizungumzia pamoja naye, utamsaidia awe mtu mzima mwenye kutegemeka.—Kanuni ya Biblia: Methali 22:6.

No comments:

Leave a Reply