Latest News


More

UNAWEZAJE KUSHUGHULIKA NA WAKWE ZAKO?

Posted by : Unknown on : Tuesday, July 21, 2015 0 comments
Unknown
Saved under :

Kushughulika na Wakwe

KIKWAZO

“Mke wangu aliwaambia wazazi wake tulipokuwa tukikabili matatizo. Kisha baba yake akanipigia simu ili kunishauri jinsi ya kushughulikia hali hiyo. Sikufurahia jambo hilo!”—James. *
“Mara nyingi mama mkwe husema, ‘Ninamkosa sana mwana wangu!’ Husema pia jinsi walivyokuwa karibu na mwana wake, jambo linalonifanya nihisi hatia kwamba nilifunga naye ndoa na kumletea mama yake maumivu ya moyo!”—Natasha.
Je, inawezekana kuzuia hali ya kushughulika na wakwe isiwe tatizo katika ndoa?

UNACHOPASWA KUJUA

Ndoa huanzisha familia mpya. Biblia inasema kwamba mwanamume anayefunga ndoa “atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” Mke pia anafanya hivyo kuelekea wazazi wake na mume wake. Anapofunga ndoa, Biblia inasema kwamba wawili hao wanakuwa “mwili mmoja.” Wanaanzisha familia mpya.—Mathayo 19:5.
Ndoa yako inachukua nafasi ya kwanza badala ya wazazi wako.Mshauri wa ndoa, John M. Gottman aliandika hivi: “Jukumu moja la msingi katika ndoa ni kwa mume na mke kuwa na umoja. Kuanzisha au kuchochea hisi hiyo ya kufanya mambo kwa umoja na mwenzi wako huenda kukatia ndani kutoshughulika sana na watu wa familia zenu.” *
Huenda ikawa vigumu kwa baadhi ya wazazi kuzoea badiliko hilo.Mume mmoja kijana anasema hivi: “Mara nyingi mke wangu alitanguliza kutimiza mahitaji ya wazazi wake kabla ya ndoa yetu. Baada ya kufunga ndoa, mama yake aliona kwamba nafasi yake imechukuliwa. Haikuwa rahisi kwake kukubali hilo.”
Huenda ikawa vigumu pia kwa baadhi ya wenzi wa ndoa wapya.James aliyenukuliwa mwanzoni anasema hivi: “Kuwa na wakwe si sawa na kuwa na marafiki unaochagua. Ni sawa na mtu fulani akuambie, ‘Umepata marafiki wawili wapya, iwe unapenda au la.’ Hata kama wanakuudhi bado ni sehemu ya familia yako!”

 UNACHOWEZA KUFANYA

Ikiwa wewe na mwenzi wako hamwelewani inapohusu jinsi ya kushughulika na wakwe, jitahidini kurekebisha tatizo hilo kwa pamoja. Fuateni ushauri huu wa Biblia: ‘Tafuteni amani, na kuifuatia.’—Zaburi 34:14.
Ili kufanya hivyo, fikiria hali zifuatazo. Kila hali inaonyesha mtazamo wa mume au mke. Hata hivyo, wote wawili wanakabili changamoto zilezile na kanuni zitakazoonyeshwa zinaweza kuwasaidia kushughulika na wakwe.
Mke wako anasema kwamba angefurahi ikiwa ungekuwa na uhusiano mzuri na mama yake. Lakini unaona ni vigumu kushughulika na mama yake.
Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mke wako kuhusu tatizo hilo na uwe tayari kufanya marekebisho. Jambo kuu si namna unavyohisi kuhusu mama-mkwe bali jinsi unavyohisi kuhusu mwenzi wako uliyeapa kwamba utampenda. Wakati wa mazungumzo mwambie njia moja au mbili hususa utakazotumia kuboresha uhusiano wako na mama yake na ujitahidi kufanya hivyo. Kadiri anavyoona jitihada zako, mke wako atakuheshimu zaidi.—Kanuni ya Biblia: 1 Wakorintho 10:24.
Mume wako anasema kwamba unawahangaikia zaidi wazazi wako kuliko yeye.
Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mume wako kuhusu tatizo hilo ili kujua maoni yake. Ni kweli kwamba mume wako hahitaji kuwa na hofu ya namna hiyo ikiwa unawaheshimu wazazi wako. (Methali 23:22) Hata hivyo, unahitaji kumhakikishia kupitia maneno na matendo yako kwamba bado unamthamini sana. Akiwa na uhakika huo, mume wako hatahisi kwamba anashindana na wazazi wako ili tu umthamini.—Kanuni ya Biblia: Waefeso 5:33.
Mke wako anaomba ushauri kwa wazazi wake badala ya kukuomba wewe.
Jaribu kufanya hivi: Zungumza na mke wako na mkubaliane kuhusu mambo ambayo mnaweza kuomba ushauri wa wazazi. Jitahidi kuwa mwenye kukubali sababu. Je, mara zote ni vibaya kuongea na mzazi kuhusu tatizo fulani? Ni wakati gani unaofaa wa kuzungumza nao? Mkikubaliana kuweka mipaka yenye usawaziko, hali hiyo haitakuwa tatizo. —Kanuni ya Biblia: Wafilipi 4:5.

No comments:

Leave a Reply