Je, michezo ya kompyuta inakuibia
wakati?
“Ninapoanza kucheza, inakuwa vigumu sana
kuacha. Mimi hujiambia, ‘Acha niendelee kidogo tu!’ Kisha bila kujua, saa kadhaa
zinapita na ninajikuta nimecheza kwa muda mrefu
sana!”—Annette.
“Michezo ya kompyuta inaweza kukupotezea muda
mwingi sana. Unakaa mbele ya kompyuta na kuhisi kwamba umetimiza jambo fulani
kwa sababu umeshinda mara tano, lakini ukweli wa mambo ni kwamba hujatimiza
jambo lolote.”—Serena.
Jambo kuu: Mtu anapopoteza
pesa, huenda akazipata tena. Lakini sivyo ilivyo unapopoteza wakati.
Kwa njia fulani, wakati una thamani kubwa zaidi hata kuliko pesa. Kwa hiyo
usiruhusu chochote kikuibie wakati wako!
● Biblia inasema: “Endeleeni kutembea kwa
hekima . . . , mkijinunulia wakati unaofaa.”
—Wakolosai 4:5.
Je, michezo ya kompyuta imeathiri jinsi
unavyofikiri?
“Matendo ya uhalifu ambayo yanaweza kumfanya
mtu afungwe gerezani au ahukumiwe kifo, yanafanywa katika michezo ya kompyuta
bila wasiwasi.”—Seth.
“Michezo mingi ya kompyuta inahusisha
kuwaangamiza maadui ili mtu apate ushindi. Kwa kawaida, kuna njia kadhaa za
kuwaua maadui kwa ukatili.”—Annette.
“Nyakati nyingine huwezi kuamini kile
unachowaambia marafiki wako mnapocheza—unawaambia ‘Kufa!’ au ‘Nitakuua
wewe!’ ”—Nathan.
● Biblia inaonyesha kwamba Yehova anamchukia
“mtu yeyote
anayependa jeuri”
—si lazima mtu awe ametenda
kwa jeuri. (Zaburi 11:5) Hata ingawa michezo ya
kompyuta unayochagua haiamui utakuwa mtu wa aina gani, michezo hiyo inaweza
kufunua mambo fulani kukuhusu au jinsi ulivyo.
Fikiria jambo hili: Kulingana na kitabu
kinachoitwa,
Getting to Calm, “michezo ya kompyuta yenye jeuri huathiri
sana tabia ya mtu hata kuliko kutazama televisheni, kwa sababu watoto
hawamtazami tu shujaa fulani mkatili anayewaua wengine ovyoovyo, bali wao
wenyewe wanakuwa ndiye shujaa mwenyewe anayetekeleza mauaji hayo. Kwa kuwa
michezo hiyo humfunza mtu kama mwalimu anavyofanya darasani, basi kihalisi mtu
hujifunza kuwa mjeuri anapoicheza.”
—Linganisha Isaya 2:4.
No comments: