Katika miaka ya hivi karibuni, maisha ya
familia katika nchi za Magharibi yamebadilika sana. Zamani watoto walitii
mwongozo wa wazazi wao. Leo, katika familia nyingi inaonekana kwamba watoto
wanawaongoza wazazi wao. Kwa mfano, fikiria hali zifuatazo zinazoonyesha jinsi
hali ilivyo.
-
Mvulana wa miaka minne yuko dukani pamoja na
mama yake, na anachukua kigari cha kuchezea. Mama yake anamkataza kwa kusema:
“Si una vifaa vya kutosha vya kuchezea?” Hata hivyo, anatambua kwamba
hakupaswa kumwuliza swali hilo. Mvulana anajibu huku akilia
“ninataka hiki!” Akijua kwamba mwana wake ana kawaida ya kulipuka kwa
hasira, mama huyo anamruhusu achukue.
-
Msichana mwenye umri wa miaka mitano anakatiza
mazungumzo kati ya baba yake na mtu fulani. Anamwambia hivi: “Nimechoka
kusubiri, nataka kwenda nyumbani!” Hata kabla baba yake hajamaliza alichokuwa
akisema, anainama na kumweleza binti yake hivi kwa sauti ya upole: “Binti yangu
mpendwa, subiri tu kwa dakika chache, sawa?”
-
James mwenye umri wa miaka 12 ameshtakiwa tena
kuwa amemfokea mwalimu wake. Baba ya James amemkasirikia sana mwalimu wa James.
“Mwalimu huyo amezoea kukusumbua,” anamwambia James. “Nitamshtaki kwenye kamati
ya shule!”
Hali hizo ni za kuwaziwa tu, ingawa kwa kweli
zinaweza kutokea kihalisi. Zinaonyesha tatizo kubwa katika familia ambazo wazazi
huruhusu watoto wajiendeshe bila adabu, hukubaliana na chochote wanachotaka, na
hata huwatetea wanapojiendesha kwa njia isiyofaa. Kitabu The Narcissism
Epidemic, kinasema hivi: “Limekuwa jambo la kawaida kuona wazazi wakikosa
kutumia mamlaka yao kuelekea watoto wao. Miaka michache iliyopita, watoto
walijua ni nani alikuwa mwenye mamlaka, nao walitii.”
Ni kweli kwamba wazazi wengi hujitahidi
kufundisha watoto wao maadili yanayofaa kwa kuwawekea mfano mzuri na kwa
kuwarekebisha kwa njia ya upendo wanapokosea. Hata hivyo, kulingana na kitabu
kilichonukuliwa hapo mwanzoni, wazazi wanaotambua faida za kufanya hivyo,
wanaonwa “kana kwamba wanapinga tamaduni za kwao.”
Kwa nini mambo yamebadilika hivyo? Kwa nini
watoto wamekosa adabu?
No comments: