Tatizo. Imeonekana
kwamba vijana wengi huwa hawajajitayarisha kukabiliana na matatizo
wanapoanza kufanya kazi. Wengine huvunjika moyo sana wanapochambuliwa
kidogo tu. Wengine hawakubali kufanya kazi yoyote isipokuwa ile
inayowapendeza. Kwa mfano, katika kitabu Escaping the Endless Adolescence, Dakt. Joseph
Allen anasimulia kuhusu kijana mmoja ambaye alimwambia hivi alipokuwa
akimhoji kwa ajili ya kazi fulani: “Ninaona kwamba sehemu fulani za kazi
hii zinaweza kunichosha, nami sitaki kuchoka.” Dakt. Allen anaandika
hivi: “Inaonekana hakuelewa kwamba kazi zote huwa na mambo fulani yanayochosha. Mtu anawezaje kuwa na umri wa miaka 23 na asijue jambo hilo?”
Kisababishi ni nini? Katika
miaka ya hivi karibuni, wazazi wengi wameamua kuwalinda watoto wao
kutokana na matatizo ya aina yoyote. Kwa sababu hiyo, binti yao
anapopata alama za chini katika mtihani, wazazi huingilia kati na
kumlazimisha mwalimu ampe alama za juu. Au, mwana wao anapoharibu kitu
fulani anapocheza, wazazi huingilia na kumlipia. Au mwana wao
anapozozana na rafiki yake, wazazi humlaumu rafiki yake.
Ingawa ni jambo la kawaida kutaka kuwalinda watoto wako, unapowalinda kupita kiasi unaweza
kuwafunza jambo lisilofaa—kwamba hawahitaji kuwajibika kwa matendo yao.
“Badala ya kujifunza kwamba wanaweza kukabiliana na uchungu na mambo
yanayokatisha tamaa, na kujifunza jambo fulani kutokana nayo,” kinasema
kitabu Positive Discipline for Teenagers, “watoto [hao] huwa
watu wazima ambao ni wenye ubinafsi sana, wakiwa na maoni ya kwamba kila
mtu, kutia ndani wazazi wao, wanapaswa kuwatimizia mahitaji yao.”
Biblia inasema nini? Matatizo ni sehemu ya maisha. Kwa kweli Biblia inasema: “Mambo mabaya huwapata watu wote!” (
Mhubiri 9:11,
Easy-to-Read Version) Hilo linatia ndani watu
wazuri. Kwa
mfano, Paulo, mtume Mkristo alivumilia matatizo ya aina mbalimbali
alipokuwa akihubiri. Hata hivyo, kukabiliana na matatizo hayo kulimletea
faida! Aliandika hivi: “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika
hali zozote nilizo nazo. . . . Nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na
pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya
kupatwa na uhitaji.”—
Wafilipi 4:11, 12.
Mambo unayoweza kufanya. Ukizingatia ukomavu wa watoto wako, jitahidi kufuata kanuni hii ya Biblia: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” (
Wagalatia 6:5)
Mwana wako akiharibu kitu fulani anapocheza, ingefaa umwache alipie
kitu hicho. Binti yako akipata alama za chini katika mtihani, huenda
hilo litaamsha fikira zake na atajitayarisha vizuri wakati ujao. Mwana
wako akizozana na rafiki yake, mfariji—lakini kwa wakati unaofaa msaidie
ajichunguze kwa kujiuliza, ‘Ninapotafakari hali iliyotokea, je,
nilichangia kwa njia yoyote mzozano huo?’ Watoto ambao hujifunza kutatua
matatizo yao huwa imara na wanajiamini zaidi—sifa ambazo hawatajifunza
ikiwa mtu fulani atawatatulia matatizo yao kila wakati.
“Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi.”—Wagalatia 6:4
No comments: